Kaimu Kocha Mkuu wa Kikosi cha Simba SC Juma Ramadhan Mgunda amesema analazimika kufanya mabadiliko ya mara kwa mara katika safu ya ulinzi kutokana na changamoto ambazo haziepukiki.

Kocha Mgunda alikabidhiwa jukumu la kukaimu nafasi ukuu wa Benchi la ufundi Simba SC, siku chache baada ya kuondoka kwa Kocha kutoka nchini Serbia Zoran Maki kwa mkataba wake kuvunjwa kwa makubaliano maalum.

Mgunda amesema anaendelea kuisuka safu yake ya ulinzi, lakini hadi sasa hajapata mtu sahihi wa kuanza katika kikosi cha kwanza kutokana na wachezaji wote wanaocheza nafasi hiyo kuwa na uwezo wa kupambana.

Amesema alipoanza kazi klabuni hapo, alilazimika kuendeleza alipoachia Kocha Zoran Maki, lakini alikua hana budi kufanya mabadiliko ya kumtumia Beki kutoka nchini Kenya Joash Onyango kutokana na majeraha yaliomkabili Henock Inonga Baka kwenye mchezo wa Mkondo wa Kwanza wa Ligi ya Mabingwa Barani Afrika dhidi ya Nyasa Bog Bullet.

“Ni kweli tangu nimeingia Simba bado sijapata kikosi cha kwanza hasa kwenye eneo la mabeki, na kama unavyojua timu huwa hazifanyi mabadiliko ya mara kwa mara kwenye eneo hilo, lakini kwangu nimelazimika kubadili kutokana na changamoto ambazo siwezi kuzikwepa,”

“Mechi ya kwanza niliendeleza pale nilipoachiwa na kocha Zoran Maki kwa kuwatumia mabeki Inonga na Ouattara, lakini alipopata maumivu nililazimika kumuingiza Onyango ambaye alikuwa nje ya timu muda mrefu.”

“Kwa sasa kila mchezaji ana nafasi ya kucheza nawatumia kulingana na kile wanachonionyesha mazoezini kabla ya mchezo.” amesema Mgunda baada ya kukishuhudia kikosi chake kikipambana na Malindi jana Jumapili (Septemba 25) mjini Unguja-Zanzibar.

Katika mchezo huo Kocha Mgunda aliwatumia mabeki Kennedy Juma na Eransto Nyoni, huku akiwaweka Benchi Mabeki Joash Onyango na Mohamed Ouattara.

Mchezo uliopita dhidi ya Nyasa Big Bullet uliopigwa Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam, Kocha huyo wa zamani wa Coastal Union ya Tanga, aliwatumia Mabeki Henock Inonga na Kennedy Juma.

Al Hilal kuweka kambi DR Congo
Cedric Kaze: Tuna uwezo wa kushinda popote