Kocha Mkuu wa Simba SC Roberto Oliveira ‘Robertinho’, amewaambia mabosi wa timu hiyo anataka ashirikishwe katika kila hatua ya usajili watakaofanya kuelekea msimu ujao baada ya kukabidhi faili la majina ya wachezaji anaowataka kwenye kikosi chake.

Robertinho ametoa kauli hiyo kufuatia Simba SC kukosa makombe yote msimu huu licha ya kuonyesha upinzani mkali mbele ya wapinzani wao Young Africans.

Young Africans wamefanikiwa kushinda ubingwa wa Ligi Kuu Bara kwa mara ya pili mfululizo huku wakifanikiwa kuingia Fainali ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika na Kombe la Shirikisho Tanzania Bara ‘ASFC’.

Robertinho amesema anataka ashirikishwe kwenye hatua ya usajili ili kupata wachezaji anaowataka kwenye kikosi chake kwa ajili ya msimu ujao watakaomwezesha kufikia malengo.

Msimu huu Simba SC walikuwa na malengo ya angalau kucheza hatua ya nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika pamoja na kuchukua ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara na kombe la Shirikisho (FA), hata hivyo wameshindwa kufikia malengo hayo na kushuhudia watani zao, Yanga wakichukua ubingwa wa Ligi Kuu na kutinga hatua ya fainali katika michuano ya Shirikisho Afrika na ile ya ASFC.

“Nashukuru Mungu kwa sasa tunasubiria kumaliza msimu kwa mechi mbili zilizobakia kabla ya kuanza maandalizi ya msimu ujao, ingawa tumeanza mikakati mapema ya kujua mahitaji gani ambayo tunaweza kuyahitaji kuelekea msimu ujao kwa sababu msimu huu hakuna ambacho tumeweza kukipata.

Kuhusu suala la usajili tayari tumeanza mikakati kwa sababu tunaelewa tumekosea wapi na kitu gani tunapaswa kufanya ili tuweze kuwa bora msimu ujao hivyo ni jambo jema kuweza kutambua kila hatua ya usajili wa wachezaji ambao tumelenga kuwasajili kupitia viongozi na ripoti itakavyoweza kuonyesha mahitaji yetu ya msimu ujao,” amesema Robertinho.

Amesema kwa sasa wanaangalia michezo miwili iliyobakia na amewataka wachezaji wake kupambana kushinda mechi mbili zilizosalia ili kumaliza ligi hiyo kwa heshima.

Kikosi cha Simba SC kimepewa mapumziko ya siku kadhaa kisha kitarejea katika uwanja wa Mo Simba Arena kuendelea na maandaa na michezo miwili ya Ligi Kuu dhidi ya Polisi Tanzania utakaopigwa Juni 6 na ule dhidi ya Coastal Union utakaochezwa Juni 9, michezo yote itachezwa jijini Dar es salaam.

Nyakua TV inch 55 kupitia Kasino mtandaoni ya Meridianbet
Viongozi 10 waliozibeba nchi zao Afrika – 3, Kwame Nkrumah 1