Kocha Mkuu wa Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ Adel Amrouche ni kama amempiga kijembe mpinzani wake Kocha wa Timu ya Taifa ya  Uganda Micho, baada ya kuibuka na ushindi wa 1-0, jana Ijumaa (Machi 24) katika Uwanja wa Suez Canal, mjini Ismailia nchini Misri.

Miamba hiyo ya Afrika Mashariki ilikutana katika mchezo wa Mzunguuko watatu wa Kundi F. wa kuwania kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika ‘AFCON 2023’ huku Uganda wakiwa wenyeji wa mchezo huo kufuatia nchi yao kukosa viwanja vyenye sifa zinazoendana na vigezo vilivyowekwa na Shirikisho la Soka Barani humo ‘CAF’.

Kocha Amrouche ambaye alikuwa katika mtihani wake wa kwanza tangu alipotangazwa kuwa Kocha Mkuu wa Taifa Stars mapema mwezi Machi, amesema alifanya maandalizi ya kutosha kuelekea mchezo huo ambao amekiri ulikua mgumu.

Kocha huyo kutoka nchini Algeria amesema mara zote amekuwa na Falsafa za kujiandaa kwa kuepuka matokeo ya sare ama kupoteza, na ndicho kilichotokea katika mchezo dhidi ya Uganda jana Ijumaa (Machi 24).

 “Tulifanya maandalizi ya kutosha kuikabili Uganda, nimekuwa na falsafa za kujiandaa kwa kukwepa matokeo ya sare ama kupoteza, ndicho kilichotokea katika mchezo wetu hapa Misri.”

Katika hatua nyingine Kocha Amrouche amewashukuru mashabiki wa Tanzania waliojitokeza kuishangilia Taifa Stars, katika mchezo dhidi ya Uganda, huku akifichua siri ya kukubali kufundisha timu hiyo kwa kusema amekua akivutiwa na ushawishi wa mashabiki ambao siku zote hujitokeza kuwapa morari wachezaji.

“Ninapenda kuwashukuru sana mashabiki waliojotokeza kuishangilia Taifa Stars hapa Misri, kwa sababu walionesha kuwa na Imani wakati wote na walifanikisha suala la kuwapa morari wachezaji wangu ili wapambane na kupata matokeo.”

“Nilifanya maamuzi ya kuja kufundisha soka Tanzania kwa sababu ya mashabiki, nimekuwa nikiona timu za hapa zinapocheza mashabiki wamekua mstari wa mbele kutoa ushirikiano wa kutosha kwa sababu wanapenda soka.”

Licha ya Rekodi ya Taifa Stars kutokuwa bora dhidi ya Uganda (kabla ya mchezo wa jana timu hizo zilikuwa zimekutana 59, Uganda ikishinda Michezo 32, Tanzania ikishinda 12, na sare 15) lakini bado mchezo wamzunguuko wanne wa Kundi F. utakaopigwa Jumanne (Machi 28) katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam ni muhimu na utakuwa wa kwanza kati ya mitatu iliyochezwa ili kukamilisha hatua ya makundi, mchezo mwingine utakuwa dhidi ya Niger na mwingine utapigwa ugenini dhidi ya Algeria.

Kwa kuwa Niger ina alama 2, hii ina maana kwamba Taifa Stars ikitumiamia vyema mchezo ujao dhidi ya Uganda itakuwa katika nafasi nzuri ya kufanikiwa, hasa kwa kuwa mchezo ujao dhidi ya Niger utacheza tena dhidi ya vinara Algeria, ambao wana nafasi kubwa ya kushinda na ikiwa hivyo itakuwa ni matokeo mazuri kwa Tanzania.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Pindi Chana mwanzoni mwa juma hili alisema serikali itatoa Sh500 milioni kwa Taifa Stars endapo itafuzu, ikiwa ni sehemu ya motisha kama ilivyofanya mara ya mwisho mwaka 2019.

Huu ni mwendelezo wa Serikali chini ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kuendelea kutoa motisha baada ya kununua kila bao kwa Shilingi milioni 5 kwenye michuano ya kimataifa kwa timu za Simba SC na Young Africans.

Kiu ya mashabiki ni kuona kikosi cha Taifa Stars kinakuwa na mwendelezo mzuri baada ya kufanya hivyo kule nchini Misri chini ya aliyekuwa Kocha Mkuu Mnigeria, Emmanuel Amunike, ambaye aliiongoza kufuzu kwa mara ya pili kihistoria ikiwa imepita miaka 39 tangu ilipofuzu kwa mara ya kwanza mwaka 1980.

Wizara Madini, Maliasili kuandaa miongozo uchimbaji Hifadhini
Kocha Dar City atamba Ligi ya RBA