Aliyekuwa mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM, Frederick Mwakalebela amefungua kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa Ubunge wa jimbo la Iringa mjini yaliyompa ushindi Mchungaji Peter Msigwa wa Chadema huku akiitaja kofia ya M4C katika shtaka lake.

Msajili msaidizi wa mahakama kuu ya kanda ya Iringa , Ruth Massama amesema kuwa Mwakalebela alifungua shtaka hilo mahakamani hapo Oktoba 30 mwaka huu.

Katika shitaka hilo, pamoja na mambo mengine, Mwakalebela anamtuhumu Msigwa kwa kuvunja sheria ya uchaguzi kwa kuvaa kofia yenye nembo ya M4C inayotumiwa na Chadema,  katika siku ya kupiga kura.

Kadhalika, mlalamikaji huyo anamtuhumu mwangalizi wa uchaguzi kwa kukiuka sheria na kanuni za uchaguzi wakati wa zoezi la kupiga na kuhesabu kura.

Katika madai yake, Mwakalebela ameeleza kuwa katika kata ya DaboDabo alikataliwa kuingia katika kituo cha kupigia kura wakati wakati mshindani wake huyo aliruhusiwa kuingia bila kizuizi chochote.

Msimamizi wa uchaguzi katika jimbo la Iringa Mjini alimtangaza Mchungaji Peter Msigwa kuwa mshindi wa nafasi hiyo hivyo kupata nafasi ya kuendelea kuliwakilisha jimbo hilo kwa muhula wa pili.

Diamond Azungumzia Mpango Wa Kuingia Kwenye Bongo Movies
Video Ya Joh Makini Na AKA Wa Afrika Kusini Kutambulishwa MTV Leo