Korea Kaskazini imesema kuwa itaharibu kabisa vinu na maeneo yaliyokuwa yametengwa kwa ajili ya majaribio ya silaha za kinyuklia wiki mbili zijazo katika sherehe itakayohudhuriwa na waandishi wa habari wa kimataifa.

Serikali inayoongozwa na Kim Jong-un imesema kuwa inaendelea kuchukua hatua za kiusalama ili kutekeleza uamuzi wake huo kati ya tarehe 23 na 25 mwezi huu, kwa mujibu wa shirika la habari la KCNA.

Hatua hiyo itafanyika wiki tatu kabla ya mkutano kati ya Kim Jong-un na Rais wa Marekani, Donald Trump uliopangwa kufanyika nchini Singapore.

Taarifa hii ya uamuzi wa Korea Kaskazini iliwahi kugusiwa na Korea Kusini ambao walieleza kuwa katika mazungumzo kati ya viongozi wa nchi hizo, Kim Jong-un aliahidi kuviharibu vinu hivyo.

Korea Kaskazini wamesema kuwa watawaalika wataalam wa nyuklia kutoka Korea Kusini na Marekani kushuhudia tukio hilo.

Korea Kaskazini imeendelea kuchukua hatua za kuachana na mpango wake wa kufanya majaribio ya silaha za kinyuklia na kuondoa mgogoro uliokuwepo kati yake na Marekani pamoja Korea Kusini kuhusu majaribio hayo.

Hivi karibuni iliwaachia huru wafungwa watatu raia wa Marekani iliyokuwa ikiwashikilia kwa tuhuma za kufanya upelelezi au kuhujumu serikali ya nchi hiyo walipokuwa wanafanya kazi nchini humo.

 

Magazeti ya Tanzania leo Mei 13, 2018
Serikali kulipasua kati jimbo la Mbagala