Mbunge wa jimbo la Ubungo kwa tiketi ya Chadema, Saed Kubenea amekanusha taarifa zilizosambaa kwenye baadhi ya vyombo vya habari na mitandao ya kijamii zinazomhusisha na wizi wa kompyuta mpakato (laptop) ya Profesa Ibrahim Lipumba pamoja na kutumia jina la nduguye aliyesoma kufanya kazi ya uandishi wa habari. Pamoa na tuhuma nyingine nzito dhidi yake.
Hili ni tamko la Kubenea: 
NIMESOMA andishi la anayejiita Seif Rashid, lililochapishwa kwenye mitandao kadhaa ya kijamii, pamoja na baadhi ya magazeti.
Andishi limejielekeza katika kunijadili binafsi: Jinsi nilivyofanikiwa kuwa mbunge wa jimbo la Ubungo, kuwa mmiliki wa kampuni ya Hali Halisi Publishers Limited – wachapishaji wa MwanaHALISI – gazeti ambalo mimi ndiye mtendaji wake mkuu – na mengine mengi.
Andishi hili lilipewa vichwa vya maneno tofauti, kulingana na mahitaji ya mchapishaji.
Kuna baadhi ya maeneo lilipewa kichwa cha maneno, “Saed Kubenea: Ndumilakuwili mbobezi.” Pengine ililiandikwa, “Mfahamu Saed Kubenea, mbunge wa Ubungo.”
Kote lilikochapishwa andishi lile, lilibeba aya kadhaa kutoka kwenye makala niliyoandika na kuchapishwa katika gazeti la MAWIO, toleo la Alhamisi ya 24 Desemba 2015.
Makala katika MAWIO ilikuwa inajadili ndimi mbili za Kiongozi Mkuu wa ACT- Wazalendo, Zitto Zuberi Kabwe.
Mwandishi anasema, nimeamua kumshambulia Zitto, kwa sababu nataka kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) ambayo Zitto pia anaitaka tena.
==>Baada ya kuisoma na kuirejea tena na tena, napenda kueleza yafuatayo:
Ni kweli kwamba Saed Kubenea ndilo jina langu. Ni kweli kuwa mimi ni mbunge wa Ubungo kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Ni kweli kwamba niliwahi kuandikia magazeti ya Mtanzania na RAI – hakuna lisilo la kweli. Basi. Yaliyobaki katika andishi la anayejiita Seif Rashid, ni uongo wa moja kwa moja, porojo au tuhuma zenye nia ya kunidhalilisha na kunivunja moyo.
Niseme hapa mapema kuwa, mimi siyo mtu wa kuvunjika moyo pale ninapokuwa nimeamua kufanya jambo. Mimi sitishwi na uongo, uzushi, porojo au suto za kwenye magenge ya kahawa au bao.
Alichokifanya anayejiita Seif Rashid, ni kuokoteza huku na kule na kutaka kuaminisha umma kuwa ni ukweli. Kwa mfano, sijawahi kutamka mahali kokote kuwa nataka kuwa mwenyekiti wa PAC.Spika wa Bunge hajapanga nani awe kamati hii au ile. Wala haijafahamika kuwa nitakuwa mjumbe wa kamati ipi.
Hata kama nitataka kuwa mwenyekiti, bado siwezi kutumia kalamu yangu kujipigia kampeni. Siamini katika siasa za aina hiyo.
Mwenye andishi anasema, ninatumia cheti cha ndugu yangu aishiye Bagamoyo na mwenye jina la Said (sio Saed); na kwamba mimi siitwi Saed Kubenea. Hataji jina langu.
Hata hivyo, ni vema nieleze yafuatayo: Jina la Saed Kubenea, ndiyo jina halisi nililopewa na wazazi wangu. Nimelirithi kutoka kwa babu yangu. Anaitwa, Saed Mohammed Kubenea. Aidha, hakuna kaka au ndugu yangu yeyote anayeishi Bagamoyo. Hayupo.
==>Nimesoma kwa kadri Mwenyezi Mungu alivyonisaidia. Nilimaliza Kidato cha Nne. Nikaanza kujifunza mwenyewe na baadaye kupata msaada wa watu mahili kunifundisha taratibu uandishi wa habari. 
==>Nikahudhuria mafunzo mafupi hapa na pale nchini. Hatimaye nikapata mafunzo ya juu ya uandishi wa habari nchini Uholanzi na India. Ninaendelea kujifunza na elimu haina mwisho.
Jingine la kugusia ni madai kuwa nilihusika na upoteaji wa anachoita, “kompyuta mpakato (laptop) ya Prof. Ibrahim Lipumba mwaka 2005.”
Suala hili liliwahi kuelezwa pia na Didas Masaburi, aliyekuwa mshindani wangu katika mbio za ubunge jimboni Ubungo.
Ukweli ni huu: Prof. Lipumba hajawahi kuibiwa kompyuta (laptop) akiwa na mimi. Kilichoibiwa akiwa na mimi ni modemu inayotumika kwa ajili ya kupata huduma ya intaneti. Bali kompyuta inayodaiwa kuwa ya Prof. Lipumba ilikuwa ni mali yangu. Siyo ya Prof. Lipumba kama ambavyo wahusika wanataka kuaminisha umma.
Kuna hili la gazeti la Hali Halisi ambalo mwandishi anasema, nilipewa mtaji na Prof. Lipumba na baadaye likatumika kama gazeti rasmi la kambi ya upinzani bungeni. Mimi sikuanzisha gazeti hili. Lilianzishwa na wabunge wa upinzani mwaka 2003. Kiongozi wa Kambi ya Upinzani alikuwa Willifred Lwakatare, mbunge wa Bukoba Mjini wakati huo.
Ninashangaa mtuhumu anapopata taarifa kwamba kufa kwa gazeti la Hali Halisi, kulinifanya kuwa na maisha magumu; na kwamba kwa huruma, Zitto Kabwe na mwenzake, Halima Mdee, wakanipa mtaji wa kuanzisha gazeti la MwanaHALISI. Hii siyo kweli na aliyeandika hivyo anajua si kweli.
Kampuni ya Hali Halisi Publishers Limited ilianzishwa 31 Januari 2005. Wakati huo Zitto na Mdee hawakuwa wabunge. Zitto na Halima hawakushiriki kwa namna yoyote ile katika kuanzisha gazeti hili. Mdee akiulizwa juu ya hili ataeleza. Hata Zitto anajua vema; na akiwa mkweli, atasema hivyohivyo. Historia isipotoshwe.
Gazeti la MwanaHALISI limeanzishwa na mimi kwa ushirikiano mkubwa kutoka kwa Absalom Kibanda na baadhi ya waandishi wengine mahiri. Labda niseme hivi, kwamba anayetaka kujua historia yangu, ya vyombo vyangu vya habari na maisha yangu ya mapambano; afanye ahadi na mimi, tukae, aniulize, nimweleze ili apate ukweli na usahihi juu yangu na kazi yangu, na hata ubunge wangu.
Hebu niweke wazi jambo hili: Kwanza, sijawahi kuwa na urafiki, kwa maana halisi ya urafiki, na Zitto. Kilichokuwepo ni ukaribu tu kama ilivyo kwa watu wengine mnapokuwa pamoja.
Pili, sishindani na Zitto. Katika lipi? Kila mmoja ana taaluma yake; na taaluma hizi zaweza kufanya kazi nzuri na vizuri kama hakutakuwa na unafiki, uzandiki na undumila kuwili kama nilioueleza katika makala yangu.
Tatu, siamini katika kuomba fadhila na kujikomba. Naamini katika kudai haki na kilichochangu; au ninachostahili kwa mujibu wa taratibu, kanuni, sheria na katiba. Haya hayahitahi kujikomba. Yanahitaji ujasiri na moyo wa utumishi kwa umma. Huko ndiko kwangu

Profesa Baregu Amvaa Magufuli
Serikali yamjibu Dk. Mahanga kwa kukosoa uteuzi wa Makatibu wakuu