Mkurugenzi Mtendaji wa Clouds Media Group, Joseph Kusaga amesema kwamba msiba wa Ruge hautakuwa wa majonzi kama ilivyozoeleka, bali itakuwa ni kusherehekea maisha yake kama ambavyo mwenyewe alitaka iwe.

Amesema kabla Ruge hajafariki, aliwahi kusema kuwa ikitokea siku amekufa, basi watu wasihuzunike sana, bali washerehekee maisha yake na vile alivyo vifanya wakati yupo hai.

“Kuna kitu alikuwa akisisitiza, kwamba ikitokea bahati mbaya Mwenyezi Mungu amemchukua, tu-‘celebrate’ maisha yake, tu-‘celebrate’ alivyovifanya,  kwa hiyo tutaanza maombolezo lakini yatakuwa ku-‘celebrate’ mazuri aliyoyafanya, hii alisisitiza wazi kabisa, na mimi kumpa heshima hiyo ni lazima tu-‘celebrate’ mengi mazuri aliyoyafanya”, amesema Kusaga.

Aidha, amesema kuwa Ruge amefanya mengi mazuri ambayo yalifaa kutunukiwa, huku akitoa shukrani kwa serikali kwa kuwa nao bega kwa bega, kwenye kipindi hiki kigumu kwao.

Amesema kuwa inaweza ikawa sio wakati mzuri wa kusema mengi, lakini Watanzania wanapaswa kujifunza kutoa tuzo au kitu chochote kizuri kwa mtu aliyefanya mambo mazuri, amefanya mengi mazuri kwenye tasnia ya burudani.

Ruge Mutahaba amefariki dunia jioni ya Februari 26 huko Afrika Kusini, alipokuwa akipatiwa matibabu ya figo aliyokuwa akisumbuliwa nayo.

 

Video: Majaliwa atoa neno kwenye msiba wa Ruge
Serikali ya Tanzania yaishukuru China