Mwanasiasa na aliyekuwa Mbunge wa upinzani (Chadema), kwa mara nyingine tena ameshindwa kufika nchini Tanzania na badala yake ametua Nairobi – Kenya alikotibiwa kabla ya kupelekwa Ubeligiji baada ya kujeruhiwa kwa kupigwa risasi, Septemba 2017.

Lissu amefika Nairobi kwa lengo la kuwashukuru raia wa nchi hiyo kwa kumchangia damu na zaidi ya yote kuwashukuru madaktari na manesi kwa kumpa matibabu ambayo yalisaidia kuokoa maisha yake.

Akizungumza katika mahojiano maalumu na kituo cha KTN amesema kwa sasa amepona kabisa lakini hataweza kurejea Tanzania hadi pale atakapo hakikishiwa usalama wake.

“Hali ya usalama wangu bado siyo nzuri nafikiri hakuna mtu ukiachia wale watu wasiojulikana na waliowatuma nafikiri wengine wote hawana maslahi na hawataki kuona narudi nyumbani kesho halafu kesho hiyohiyo au keshokutwa yake napigwa risasi tena”  amesema Lissu.

Lakini amesema kuwa marafiki na watu wenye busara bado wanapanga mipango kuangalia jinsi ya yeye kurudi na kuwa salama.

“Jitihada zinafanyika kwa maeneo mengi tu, marafiki zetu wa ndani na nje ya nchi wanajadiliana namna ya kuhakikisha nitakuwa salama, sasa wakifika mahali wakiniambia sasa bwana Lissu usalama wako utaangaliwa basi nitarudi nyumbani” amesisitiza Lissu.

Aidha Lissa amezungumzia pia nia yake ya kugombea katika nafasi ya Urais 2020, kwa kusema kama chama chake na vyama rafiki vya kisiasa nchini vikimpa dhamana ya kuwakilisha uchaguzi mkuu ujao yupo tayari kuitikia wito huo.

Video: Safari ya Lissu kurejea yaishia Nairobi, Mtego anguko la Sumaye Chedema
BREAKING: Hassan Mwakinyo ampiga Tinampay