Mlipuko wa roketi umesikika nje ya eneo la ubalozi wa Marekani katika mji mkuu wa Afghanistan, Kabul, punde tu baada ya saa kuonesha ni Septemba 11.

Hii ni tarehe inayokumbukwa kwa shambulizi baya zaidi kuwahi kufanyika katikati ya majiji ya Marekani na kusababisha vifo vya watu takribani 3,000, baada ya kundi la kigaidi la Al-Qaeda lililokuwa likiongozwa na Osama Bin Laden kuteka ndege na kuzigongesha kwenye majengo marefu.

Kwa mujibu wa India Today, maafisa waliokuwa eneo la ubalozi wa Marekani nchini Afghanistan wameeleza kuwa hakuna madhara yoyote yaliyojitokeza.

Moshi mkubwa umeonekana baada ya mlipuko huo kusikika, lakini Serikali ya Afghan haijazungumzia tukio hilo. Misheni ya NATO iliyo karibu na Ubalozi wa Marekani imeeleza kuwa hakuna mtu wao yeyote aliyejeruhiwa.

Mlipuko huo unadaiwa kuwa ni shambulizi kubwa zaidi ambalo halikuleta madhara jijini Kabul lililotokea siku chache tangu Rais wa Marekani, Donald Trump alipotangaza kusitisha mpango wa mazungumzo na wapiganaji wa Taliban kwa lengo la kusitisha vita ya muda mrefu.

Wiki iliyopita, Kundi la Taliban lilifanya mashambulizi kwa kutumia magari mawili yaliyosheheni mabomu, na kusababisha vifo vingi vya raia, wanajeshi wawili wa NATO na mwanajeshi mmoja wa Marekani. Rais Trump alisema kitendo hicho ni sababu ya kusitisha mpango huo wa mazungumzo.

Septemba 11, ni tarehe muhimu pia kwa kundi la Taliban na mji mkuu wa Afghanistan, kwani ni tarehe ambayo saa chache baada ya Al-Qaeda kuishambulia Marekani, vikosi vya Marekani vilifanya mashambulizi makali dhidi ya Taliban ambao wakati huo ndio waliokuwa wanaunda Serikali. Mashambulizi hayo ya Marekani dhidi ya Taliban yalitokana na sababu kuwa Osama alikuwa analitunzwa na kundi hilo.

Hata hivyo, Marekani imekuwa ikipunguza vikosi vyake nchini Afghanistan tangu Osama alipouawa mwaka 2011 nchini Pakistani.

Video: Nape alivyoteseka kumuomba radhi JPM, Faru 9 waletwa kutoka 'Sauzi'
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Septemba 11, 2019