Ule msemo wa waswahili usemao “Adui Yako Muombee Njaa” umedhihirishwa na mshambuliaji kutoka nchini Argentina na klabu bingwa Hispania FC Barcelona, Lionel Messi baada ya kuonyesha kuwa na matumaini ya kuwaona wapinzani wao Real Madrid wakimaliza msimu wakiwa mikono mitupu.

Messi ambaye aliiongoza FC Barcelona kupata ushindi wa kishindo wa mabao matano kwa sifuri mwishoni mwa juma lililopita dhidi ya Espanyol katika mshike mshike wa ligi ya nchini Hispania, amezungumza kauli hiyo alipofanyiwa mahojiano na kituo cha televisheni cha ESPN cha nchini Marekani.

Messi amesema ana imani kubwa, Real Madrid wanaonolewa na gwiji wa soka kutoka nchini Ufaransa, Zinedine Zidane wataambulia patupu mwishoni mwa msimu huu, licha ya kuwa katika mazingira mazuri ya kuwapa ushindani kwenye mbio za ubingwa wa La Liga pamoja na kutinga kwenye hatua ya fainali ya ligi ya mabingwa barani Ulaya ambapo watacheza dhidi ya Atletico Madrid, Mei 28 huko mjini Milan nchini Italia.

“Ni kawaida kwa watu wa Barcelona kuona Real Madrid hawafanikiwi katika msimu wowote, na mimi ni mmoja kati yao ambaye ninaamini kwa msimu huu hawatoondoka na chohote licha ya kuwa katika mazingira mazuri ya kuwania mataji,” Messi alizungumza katika kipindi cha ESPN

“Sisi tuna nafasi nzuri ya kushinda taji la La Liga msimu huu, kutokana na mazingira ya msimamo wa ligi ya nchini Hispania kutubeba kwa tofauti ya point moja na sio kwao, na nikuhakikishie hata katika ligi ya mabingwa barani Ulaya hawatofanya lolote, kutokana na ubora wa wapinznai wao.” Aliongeza mshambuliaji huyo anayeshikilia tuzo ya ubora wa soka duniani

Katika mchezo wa mwisho wa ligi ya nchini Hispania msimu huu ambao utachezwa mwishoni mwa juma hili na kuamua hatma ya ubingwa, Real  Madrid watapambana na Deportivo La Coruna huku FC Barceloan wakipambana na Granada CF.

FC Barcelona pia watakuwa na nafasi nyingine ya kuwania taji la mfalme msimu huu kwa kucheza dhidi ya Sevilla, mwishoni mwa juma lijalo.

Chadema wamgeuka Magufuli uhaba wa sukari, waja na haya dhidi yake
FC Bayern Munich Wazimisha Ndoto Za Man Utd