Aliyekua kocha wa timu za taifa za England na Urusi Fabio Capello, amesema hakupendezwa na kitendo cha Lionel Messi na Cristiano Ronaldo kutohudhuria hafla ya utoaji wa tuzo ya mchezaji bora wa dunia wa FIFA mwaka 2017/18.

Capello amesema kitendo cha wachezaji hao, kimeonyesha namna walivyoshiba mafanikio waliyoyapata kwa miaka kumi, ambapo walikua wakipokezana kutwaa tuzo mbalimbali duniani.

Amesema pamoja na kutoelezwa kwa kina nini kilichowakwamisha kufika katika hafla hiyo iliyofanyika jijini London, bado kulikua na sababu ya kuwepo hata wawakilishi wao, lakini haikua hivyo.

“Kushiba mafanikio wakati mwingine kunaweza kukufanya ukajiona hakuna mwingine zaidi yako, huu ni utovu wa nidhamu, ambao unaendelea kuwashusha katika medani ya soka,”

“Suala la kushinda hizi tuzo kwa muda mrefu haliwezi kukupa jeuri na kiburi hadi kufikia hatua kama hii, lakini kwa upande wangu ninaamini hili ndilo anguko lao, na sitarajii kama nitawaona tena katika harakati za kugombea tuzo kubwa duniani.” Alisema Capello ambeye pia amewahi kuzinoa klabu kubwa duniani kama Real Madrid, Juventus na AS Roma.

Katika usiku wa tuzo, kiungo na nahodha wa timu ya taifa ya Croatia Luka Modric alitangazwa mshindi, hatua ambayo ilimaliza zama za Messi na Ronaldo

Kiungo huyo wa klabu ya Real Madrid alishinda tuzo hiyo na kuwapiku wapinzani wake Cristiano Ronaldo na Mohamed Salah, waliokua wameingia kwenye tatu bora.

Rafael Benitez aponzwa na kauli yake
Jose Mourinho afichua siri ya kutolewa Carabao Cup