Uongozi wa klabu ya Liverpool umekanusha taarifa za kujiuzulu kwa Zeljko Buvac ambaye ni msaidizi namba mbili wa mkuu wa benchi la ufundi la klabu hiyo Jurgen Klopp.

Taarifa za kujiuzulu kwa Buvac zimeibuka wakati kikosi cha Liverpool kikiwa katika maandalizi ya mwisho ya mchezo wa mkondo wa pili wa nusu fainali wa ligi ya mabingwa barani Ulaya dhidi ya AS Roma, utakaochezwa keshokutwa Jumatano mjini Roma, Italia.

Sababu za kujiuzulu kwa msaidizi huyo ambaye ni raia wa Bosnia, zinaeleza kuwa hana mahusiano mazuri na bosi wake, na ameona njia sahihi ni kuachia ngazi.

“Klopp na Buvac bado wapo na watafanya kazi pamoja,” imeeleza taarifa iliyotolewa na Liverpool kukanusha uvumi uliosambaa.

“Kwa sasa Buvac ana matatizo ya kifamilia na amepewa ruhusa hadi mwishoni mwa msimu huu ili kwenda kuyakabili.”

“Zeljko atachukua jukumu wa Buvac katika kipindi hiki, na tunamaini atafanya kazi vizuri kwa kushirikiana na Klopp ambaye kwa sasa anajukumu la kuivusha timu yetu hadi kwenye mchezo wa fainali wa ligi ya mabingwa barani Ulaya.”

Buvac mwenye umri wa miaka 56, amefanya kazi sambamba na Klopp kwa muda wa miaka 17 wakianza kama wachezaji wa klabu ya Mainz 05 na baadae kupewa jukumu la kukaa kwenye benchi la klabu hiyo, kabla ya kutimkia Borussia Dortmund na baadae wakaenda wote Liverpool.

Kikosi cha Liverpool kipo katika maandalizi ya mwisho ya kujiandaa na mchezo wa mkondo wa pili wa nusu fainali, na tayari kimeshasafiri kuelekea mjini Roma kwa pambano hilo.

Katika mchezo wa mkondo wa kwanza Liverpool walichomoza na ushindi wa mabao matano kwa mawili dhidi ya AS Roma.

Zinedine Zidane: Tutashambulia mwanzo mwisho
Mbunge aomba muongozo baada ya kufinywa makalio