Siku moja baada ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi kulieleza Bunge kuwa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa alijimilikisha shamba la Makuyuni Wilayani Monduli mkoani Arusha, Mbunge wa Monduli, Julius Kalanga amejitokeza kutoa ufafanuzi unaomsafisha.

Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Dodoma, Kalanga alisema kuwa Lowassa hamiliki shamba hilo la Makuyuni kwakuwa tangu Rais wa Serikali ya Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa alipofuta hati ya umiliki wa shamba hilo kutoka kwa raia wa Kigeni aliyemtaja kwa jina la Stein, bado halijamilikishwa rasmi kwa wananchi na ndio ilikuwa hoja yake.

Alisema kuwa maelezo ya Lukuvi hayakuwa na ukweli  na kwamba alichanganya kati ya shamba hilo la Mkuyuni na shamba la Manyara Ranchi ambalo hati yake ilifutwa tangu mwaka 2000 na kukagawiwa kwa wananchi wa Monduli ambapo Lowassa alisaini hati miliki yake kama muwakilishi wa wananchi wa Wilaya hiyo kwakuwa wakati huo alikuwa Mwenyekiti wa Bodi ya udhamini ya Ardhi (Tanzania Land Trustee (TLCT).

“Jambo la kushangaza ni pale Waziri alipochanganya shamba hilo na lole la Manyara Ranchi ambalo hati yake ilifutwa tangu mwaka 2000 na kugawiwa kwa wananchi. Hati miliki ya shamba hilo [la Manyara Ranchi] ilisainiwa na Lowassa ambaye wakati huo alikuwa mwenyekiti wa Bodi ya Tanzania Land Trustee(TLCT),” anakaririwa.

Awali, Waziri Lukuvi alieleza kuwa Shamba hilo la Mkuyuni linapaswa kumilikishwa kwa wananchi lakini nyaraka zinaonesha kuwa hati yake imesainiwa na Lowassa na kwamba Serikali itamnyang’anya na kulirejesha kwa wananchi.

Jana, Lowassa aliahidi kuwasiliana na Mbunge huyo ili kufuatilia kauli aliyoitoa Waziri Lukuvi dhidi yake kuhusu kujimilikisha shamba hilo ili aweze kutoa ufafanuzi kwani hakuna ardhi anayoimiliki kinyume cha taratibu.

SEKTA YA UMEME YANEEMEKA, MAKAMPUNI 52 YAJITOKEZA KUWEKEZA
Video: Mbunge Ally Kessy Aguswa na Haya Bungeni, Aachia Ujumbe Kwa 'Style', Tazama