Hatimaye aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema anayeungwa mkono na vyama vya upinzani vinavyounda Ukawa, Edward Lowassa ametangaza kurudi nyuma na kujipanga upya kwa awamu ya pili.

Akiongea jana kwenye tafrija fupi ya kuishukuru timu yake ya kampeni pamoja na wananchi waliomuunga mkono, Lowassa aliwataka wote waliokuwa wanamuunga mkono kutokata tamaa na kujipanga upya kwani awamu ya pili inakuja.

Lowassa alieleza kuwa kilichofanyika ni sawa na kuichelewesha bahati ya mtu na kudai kuwa anachelewesha bahati ya mtu hawezi kuiondoa bali ataizuia kwa muda tu.

“Unaweza kuchelewesha bahati ya mtu, lakini hauwezi kuiondoa,” alisema Lowassa na kuisihi timu yake kushikamana na kujipanga upya. Muda wote aliokuwa akiongea timu yake hiyo pamoja na viongozi wa Ukawa walionekana kumuunga mkono na kumshangilia.

Lowassa alipinga matokeo yaliyokuwa yanatangazwa na NEC yaliyompa ushindi Dkt. John Magufuli na kuwasilisha pingamizi lake kwa Tume hiyo akiwataka kusitisha mchakato wa utangazaji wa matokeo lakini haikuwezekana. Aliituhumu Tume hiyo kwa kile alichodai kumpokonya ushindi wake na kutangaza matokeo batili kwa kumpunguzia kura na kumuongezea Dkt. Magufuli.

Alidai kuwa baada ya kufanya majumuisho ya kura kwenye vituo vyote, yeye alipata kura zaidi ya milioni 10 tofauti na idadi ya kura milioni 6 iliyotangazwa na Tume hiyo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, alieleza kuwa kwa kuwa matokeo ya urais hayawezi kupingwa mahakamani, hivi sasa hawana jinsi zaidi ya kurudi nyuma na kujipanga upya kwa ajili ya awamu ya pili.

Alisema hivi sasa watafungua kesi za majimbo 30 ya ubunge ambayo wana ushahidi kuwa yalipokonywa kibabe na CCM.

Katika hatua nyingine, Mbowe alieleza kuwa hivi sasa viongozi wa Ukawa kwa pamoja wamepanga kupiga kambi visiwani Zanzibar kuanzia wiki ijayo ili kumuongezea nguvu mgombea urais kupitia CUF, Maalim Seif Shari hamad ili wananchi wasipokonywe haki yao kwa kufutwa matokeo ya uchaguzi wanayoamini kuwa yanampa ushindi mgombea huyo wa CUF.

Maalim Seif Ataja Siku Ya Mwisho Ya Kuwaomba ZEC Na Hatua Atakayochukua
Ruby: Niliandaliwa Kucheza Mpira Wa Miguu Ngazi ya Taifa