Kocha mkuu wa Young Africans Luc Eymael amependekeza usajili wa wachezaji wanne wa kigeni kuboresha kikosi chake kwa ajili ya kuwania ubingwa wa ligi kuu msimu ujao

Mbelgiji huyo amepania kuipa Young Africans ubingwa msimu ujao, amesisitiza kuwa ili kufanikisha hilo wanahitaji kufanya usajili wa wachezaji wenye uwezo wa kufanikisha hilo

Eymael amedokeza kuwa nyota aliopendekeza wasajiliwe wanatoka Mataifa ya Afrika Kusini, Ghana na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo “Nipo Ubeligiji lakini kila kitu niliacha kwa viongozi.

Kwenye ripoti yangu nimetoa mapendekezo ya wachezaji wanne wa kigeni kutoka kwenye mataifa ya Ghana, Afrika Kusini na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo,” alisema Eymael

“Kwa msimu ujao kama kocha na benchi la ufundi tumeweka malengo ya kuhakikisha tunachukua ubingwa, hivyo ni lazima usajili wetu uendane na mahitaji ya kuwa na timu imara zaidi ya hii tuliyonayo sasa”

“Nimefanya kazi kwenye Mataifa hayo, nawafahamu wachezaji wa nchi hizo, wanatumia akili na wana kasi na uzoefu. Nadhani tukiwapata wataleta changamoto na ushindani kwenye kikosi chetu”

“Tangu nimefika Tanzania nimeiongoza Young Africans kwenye michezo kadhaa licha ya baadhi ya viwanja kuwa katika mazingira magumu kwa wachezaji lakini lazima niwe na kikosi kinachoundwa na nyota wenye uwezo binafsi kama Bernard Morisson kwa ajili ya kusaidia kupata matokeo mazuri katika michezo inayoonekana migumu”

Eymael ameshindwa kurejea nchini kutokana na zuio la kusafiri lililowekwa huko Ubelgiji kutokana na changamoto ya ugonjwa wa Corona

Aidha atakaporejea nchini, napo atakutana na amri ya kukaa karantini kwa siku 14 likiwa ni agizo lililotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk John Magufuli katika jitihada za kudhibiti maambukizi ya virusi vya Corona.

Corona: Marekani yapata vifo zaidi ya 1500 kwa siku moja
CAG aianika Wizara ya Maliasili, 'Sh 2.5 bilioni zilitumika bila utaratibu'