Kocha Mkuu wa Young Africans Luc Eymael amesema mchezo wa Nusu Fainali Kombe La Shirikisho Tanzania Bara (ASFC) dhidi ya Simba SC ambao utapigwa keshokutwa Jumapili, ni wa kufa au kupona.

Baada ya kukosa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara, kocha Eymael amesema ubingwa wa kombe La Shirikisho (ASFC) ndio utawapatia nafasi ya kushiriki michuano ya Kimataifa msimu ujao, hivyo hawana namna zaidi ya kushinda mchezo huo.

Kocha huyo kutoka nchini Ubelgiji amesema wanafahamu mchezo hautakuwa mwepesi kwa sababu unahusisha vilabu vyenye upinzani wa jadi, lakini pia matokeo ya ushindi ambao Young Africans waliyapa kwenye mchezo uliopita baina yao, unawafanya Simba SC wakamie mchezo huo wakitaka kulipa kisasi.

“Hii mechi itakuwa ngumu sana, kwa sababu Simba wanataka kulipa kisasi kwani tuliwafunga mchezo uliopita wa Ligi Kuu Tanzania Bara, lakini wote tunataka kuingia fainali na kutwaa ubingwa huu,” alisema.

“Sisi mchezo huu una umuhimu mkubwa sana kwetu, kwani inaweza ikawa njia ya kushiriki michuano ya kimataifa, na tumejiandaa tunamaliza kazi mapema,” alisema Eymael.

Baada ya ushindi dhidi ya Kagera Sugar kule Bukoba, Young Africans iliendelea kubaki mkoani humo ikijiandaa na mchezo huo, kikosi kikitarajiwa kurejea jijini Dar es salaam leo Ijumaa kwa ajili ya kukamilisha maandalizi ya mwisho.

RIPOTI: Kasi ya ukuaji uchumi wa Tanzania kufunika nchi zote Mashariki mwa Afrika
Vandenbroeck: Wasubiri makali na hasira za kikosi changu