Waziri wa mambo ya Ndani, Kangi Lugola mapema leo hii ameongea na vyombo vya habari akiwasilisha maagizo mbalimbali ambayo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli alimuagiza pindi akimuapisha mnamo Julai 2, 2018.

Leo hii Julai 21, 2018 amesema Rais Magufuli amechoshwa kutenga fedha kuwalisha wafungwa ili hali pesa hizo zinahitajika kuendeleza jamii katika sekta mbalimbali, hivyo ametoa agizo kwa wakuu wa majeshi ya gereza hapa nchini kuandaa mikakati ya kuwawezesha wafungwa kutumia nguvu zao kujitafutia chakula ili iwe sehemu ya mafunzo na kujutia kwa kile walichokifanya kwa jamii.

”Nimeelekeza Mkuu wa jeshi la magereza nchini kutengeneza mkakati maalumu utakaokwenda kuhakikisha kwamba wafungwa magereza yote wanajilisha kuanzia chakula kuanzia mboga kwa maana iwe ni nyama iwe ni samaki wafuge ili waweze kujilisha kama ni maharage mboga walime wajilishe”. amesema Lugola.

Hata hivyo amemtahadharisha mkuu wa jeshi la magereza na kumtaka asilete kisingizio chochote katika utekelezaji wa suala hilo kwani ni jambo linalowezekana.

Aidha ametoa tahadhari kwa wakuu wa magereza kuhakikisha kwamba hakuna mfungwa yeyote kuingia na vifaa visivyoruhusiwa gerezani ikiwemo simu na vifaa vinginevyo, endapo gereza lolote litabainika kuingiza vifaa hivyo mkuu wa gereza hilo atakuwa amepoteza sifa za kuwa mwajiliwa lakini pia Seriklai itamwajibisha.

Madereva, wamiliki magari wote kuswekwa mahabusu
Kalinic aigomea medali yake ya kombe la dunia