Kufuatia kuvuliwa cheo kwa aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba kutokana na ongezeko kubwa la ajali nchini na kuteuliwa kwa Kangi Lugola ambaye sasa anashika nafasi hiyo, Waziri huyo mpya tayari ameanza kazi kwa kasi hasa katika kutafuta suluhu za ajali ambazo zimekuwa zikitokea mara kwa mara.

Ambapo amesema Serikali inajipanga kuja na mbinu mpya ya kudhibiti na kupunguza ajali zinazosababishwa na pikipiki.

Lugola amesema Serikali itaanzisha utaratibu wa kufunga tela katika pikipiki kwamba abiria wataweza kupanda kati ya mmoja hadi wanne na kuketi katika tela hilo.

Kwa kufanya hivyo amesema ajali za pikipiki zitapungua kwa kiasi kikubwa sana kwani pikipiki zikishafungwa tela zitashindwa kutembea kwa mwendokasi mkubwa kutokana na uzito lakini pia zitashindwa kupenya penya barabarani na kufanya vurugu.

”Tutawafungia matela ya kubeba abiria na nyie mkae kwenye foleni kama bajaji na magari mengine. Matela haya yataleta utulivu barabarani lakini pia yatawaongezea tija kwani badala ya kubeba abiria mmoja sasa mtapakia zaidi” amesema Lugola

Ameongezea kuwa ufungwaji huo wa matela utahusisha zaidi pikipiki za biashara na hautazihusu pikipiki binafsi.

”Bodaboda dawa yenu inachemka Serikali inakuja na mpango madhubuti wa kupunguza kama si kumaliza kabisa ajali za barabarani zinazosababishwa na madereva pikipiki,” amesema Lugola.

 

Watatu mbaroni kwa wizi wa meno ya tembo
Daley Blind kurudi Ajax Amsterdam