Mshambuliaji wa Manchester United, Romelu Lukaku amemtetea kocha wa zamani wa klabu hiyo, Jose

Mourinho dhidi ya lawama anazoendelea kurushiwa.

Mchezaji huyo kutoka Ubelgiji ambaye safari yake ya kuingia Man United iliwezeshwa na kocha huyo Mreno, amesema kuwa kocha huyo anastahili heshima na pongezi kwani alifanya kazi kubwa katika misimu miwili.

Lukaku aliyasema hayo katika mahojiano na Eleven Sports, ambao walitaka awaweke kwenye mzani Mourinho aliyekuwa akijiita ‘The Special One’ na kocha mpya Ole Gunnar Solskjaer.

“Mimi sitawalinganisha mameneja hawa. Ninaamini Mourinho alifanya mengi mazuri kwa Klabu. Alishinda makombe, kwahiyo nina mheshimu sana. Ni kocha aliyenisaini mimi,” alisema Lukaku.

Solskjaer ndio ameanza safari yake hapa. Ninatumaini mambo yataenda vizuri. Ninatumani tu kuwa tutamaliza katika nafasi nne za juu na kwamba tutachukua taji,” aliongeza.

Tangu alipoingia Old Trafford, Mourinho alibeba makombe matatu katika kipindi chake cha awali.

Alipata misukosuko kwenye msimu wa pili, lakini alifanikiwa pia kurejea akiipandisha hadi nafasi nne za juu.

Hata hivyo, katika kipindi cha miaka miwili, Kocha huyo msema mengi alishindwa kunyakua kombe la Ligi Kuu.

Baada ya mambo kumuendea kombo mwanzoni mwa msimu wa 2018/19, alitimuliwa na nafasi yake kukaliwa na Solskjaer ambaye amerejesha matumaini zaidi.

Leo, Man United itaingia dimbani dhidi ya Burnley FC, kwenye mchezo wa Ligi Kuu. Wapiga soka hao wa Old Trafford wanapewa 76% ya ushindi, 16% ya sare na 8% za kupoteza. Endapo itashinda, itapiga hatua moja hadi nafasi ya tano, na kwenda bega kwa bega na Chelsea.

LIVE IKULU: Rais Magufuli akiwaapisha Majaji wa Mahakama Kuu
Video: Chadema wamtukana Kakobe, Siri nyuma ya teuzi za JPM