Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amewaagiza watumishi wa wizara hiyo katika kitengo cha huduma kwa wateja, kufanya kazi hadi usiku ili kuhakikisha wanawahudumia kwa muda wananchi wengi wanaofika katika kitengo hicho na kuondoka bila kupata huduma stahiki.

Waziri Lukuvi alitoa maagizo hayo jana alipofanya ziara katika kitengo hicho na kubaini kuwepo urasimu mkubwa unaopelekea wananchi kushindwa kupata  huduma kwa wakati. Baada ya kuzungumza na baadhi ya wananchi waliofika katika kitengo hicho, alibaini kuwepo wananchi ambao wamekuwa wakifuatilia hati zao kwa takribani miezi mitatu bila mafanikio lakini alipoagiza wapewe hati hizo zilipatikana mara moja.

“Watu wasirudi bila kuhudumiwa. Na kama ni wafanyakazi watabaki mpaka usiku, tutafanya utaratibu wa hao wafanyakazi wanaobaki mpaka usiku. Wafanyakazi wabaki muda zaidi lakini kila anayekuja katika kituo kile lazima ahudumiwe,” alisema Lukuvi.

Pia, Lukuvi aliagiza kufungwa kwa mitambo itakayosaidia kutoa huduma za kieletroniki. Alisema kuwa uanzishwe mfumo wa kuwasiliana na wananchi wanaohitaji huduma katika kitengo hicho kwa njia ya barua pepe, whatsApp, simu na kadhalika.

Naye Kaimu Katibu Mkuu wa wizara hiyo ambaye pia ni kamishna Mkuu wa ardhi, Dk Moses Kusiluka alisema kuwa katika utoaji wa huduma hukutana na changamoto inayotokana na baadhi ya watu wanaotaka kujipatia hati kwa njia za udanganyifu bila kuwa na nyaraka za kisheria husasan wanapokuja kuwawakilisha watu wengine.

 

Serikali Yawaonya Wanaoiadhibu Mifugo
CUF Yapinga Kilichosemwa na CCM kuhusu Mazungumzo ya Mgogoro wa Uchaguzi