Leo Mei 29, 2018 Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi emesema serikali itawafikisha Mahakamani na kutaifisha mali kwa wananchi wote wanaomiliki ardhi ambao wamekuwa hawalipi kodi ya ardhi.

“Natoa onyo kwa wadaiwa sugu wote wasiolipa kodi ya pango la ardhi kwamba serikali itaendelea kuwachukulia hatua kali za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwafikisha mahakamani, kuitaifisha mali zao ili kufidia kiwango cha kodi wanachodaiwa au kufutiwa hati miliki”, amesema Lukuvi.

Amezungumza hayo akiwa Bungeni Jijini Dodoma kwenye kikao cha 37 mkutano wa 11 wa Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara yake kwa mwaka wa fedha 2018/219.

Amesema kuwa mwaka huu wa fedha ambao unaishia mwezi Juni Wizara ya Ardhi ilipanga kukusanya Bilioni 112.5  itakayotokana na vyanzo vya mapato ya kodi, ada na tozo mbalimbali za ardhi.

Lukuvi amesema hadi Mei 15 wizara ilikuwa tayari imekusanya Bilioni 78.9 sawa na asilimia 70 ya lengo lililokusudiwa.

Pamoja na hayo, Waziri Lukuvi ameendelea kwa kusema “kwa hiyo natoa wito kwa wote wanaomiliki ardhi kisheria wakumbuke kulipa kodi kwa mujibu wa sheria”.

Kwa upande mwingine, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amesema bado kuna muitikio mdogo wa wananchi kumilikishwa ardhi hususan katika maeneo ya urasimishaji.

Burundi 'yawaka' Ufaransa kuwapa wanakijiji zawadi ya Punda
Nape ampa mkono Kinana, aikumbuka mbegu aliyopanda