Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa amelazimika kukatisha kuhudhuria mkutano wa Jumuiya ya Madola unaofanyika London, Uingereza ili kukabiliana na vurugu za maandamano na ghasia zilizolikumba Jimbo la Kaskazini Magharibi mwa nchi hiyo.

Polisi nchini humo walijaribu kutuliza ghasia kwa kurusha risasi za mpira Ijumaa ili kusambaratisha umati mkubwa wa waandamanaji kabla ya kuwasili kwa Rais katika jimbo la Kaskazini Magharibi ambako vurugu zimetokea.

Mapambano makali yametokea katika eneo hilo ambapo waandamanaji wanadai ajira, makazi na kutokomezwa ufisadi.

Maduka yamevunjwa na kuibiwa, barabara zimewekwa vizuizi na magari yamechomwa moto.

Rais Ramaphosa ametoa wito kuwepo utulivu na ameamrisha polisi kujizuilia.

Vyombo vya habari nchini Afrika Kusini vimeripoti kuwa maafisa wa polisi wametumia mabomu ya machozi kuwatawanya waandamanaji ambao walikuwa wamechoma moto basi, kupiga mawe magari na kuziba barabara kwa kutumia matairi yanayowaka moto.

Benki ya Dunia yaguswa na athari za mafuriko Dar
Mwili wa Masogange kuagwa Leaders, kuzikwa Mbeya