Maelfu ya watu wanaopinga sheria zilizowekwa kudhibiti covid-19 wameandamana katika jiji la Berlin nchini Ujerumani na London nchini Uingereza.

Waandamanaji hao wapatao 20,000 jijini Berlin na kundi lingine likionekana jijini London, wamepanga kuandamana hadi Brandenburg watakapokutana na waandamanaji wengine kutoka nchi za Ulaya.

CNN imeripoti kuwa baadhi ya waandamanaji walikuwa wamebeba picha za wabunge wa Ujerumani na kuandika ‘wana hatia’, wengine wakiwa na mabango yenye jumbe mbalimbali za kupinga sheria zilizowekwa kwa lengo la kudhibiti kusambaa kwa covid-19.

Hata hivyo, jeshi la polisi la Ujerumani limeandika kwenye akaunti yake ya Twitter kuwa wamewatawanya waandamanaji hao kwani wamekiuka sheria ya kuvaa barakoa na kutokusanyika.

“Kwa bahati mbaya, hakukuwa na namna nyingine, tumemfuata kiongozi wa maandamano hayo na kumueleza kuwa polisi watatawanya maandamano hayo,” Polisi wameandika Twitter.

“Tahadhali zote za awali hazijachukuliwa kwa kuzingatia mahitaji. Kutozingatia kanuzi za kupambana na covid-19 ikiwa ni pamoja na kutokusanyika,” waliongeza.

Zaidi ya askari 3,000 walipewa kazi ya kuanagalia kama maandamano hayo yalizingatia kanuni ya kuhakikisha wanapeana nafasi.

“Tunapata ushirikiano mkubwa kutoka kwa viongozi wa majimbo mengine. Tafadhali hakikisha mnapeana nafasi kila siku na mbaki salama,” Tweet ya polisi ilieleza.

Mapema wiki hii, Serikali ya Jiji la Berlin ilitangaza kuwa ingepiga marufuku maandamano hayo kutokana na hofu ya kuvunja kanuni za kupambana na virusi vya corona.

Hata hivyo, katazo hilo liliondolewa Ijumaa baada ya Mahakama ya Berlin kutoa uamuzi  wa dharura ikibatilisha katazo hilo, hadi leo hali ilipobadilika tena.

Polisi wanawashikilia watu 300 kutokana na maandamano hayo.

Wanandoa wenye umri mkubwa zaidi duniani waeleza siri ya mafanikio
Mwanamke mwenye miaka 42 akamatwa kwa kumbaka mvulana wa shule ya msingi