Watu 31 wamepoteza maisha katika kituo cha kujiandikisha kupiga kura jijini Kabul nchini Afghanistan, baada ya mtu mmoja kufyatua bomu la kujitoa mhanga.

Vyombo vya usalama nchini humo vimeeleza kuwa shambulizi hilo la kujitoa mhanga pia limewajeruhi vibaya watu zaidi ya 50.

Kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari vya Kabul, mshambuliaji aliyejifunga bomu la kujitoa mhanga alipenya katikati ya umati uliokuwa umefurika kuanzia kwenye mlango wa kuingilia, kwa lengo la kujiandikisha kuwa wapiga kura.

Kundi la kigaidi la Islamic State limetoa taarifa kupitia shirika lake la habari la Amaq likieleza kuhusika na utekelezaji wa shambulizi hilo dhidi ya watu wasiokuwa na hatia.

Shambulizi hili linasababisha idadi ya watu waliouawa kwenye mashambulizi ya kigaidi katika vituo vya kujiandikisha kupiga kura kufikia 63, kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya nchi hiyo.

Uandikishaji wa wapiga kura nchini humo umeanza rasmi mwezi huu kwa ajili ya uchaguzi wa wabunge utakaofanyika Oktoba mwaka huu.

 

Mugabe autosa mwaliko wa Rais wa Zimbabwe
Video: Salamu za Diamond, Alikiba msiba wa Masogange