Jeshi la Polisi Mkoani Kilimanjaro, limefanikiwa kukamata magari 20 yaliyoibwa nchini Kenya mwaka 2018/2019 na kutaja wilaya nne za mkoa huo kuwa zilitumika kama uchochoro wa kuyaingiza Tanzania magari hayo.

Hayo yamesemwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Hamis Issah alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, ambapo amezitaja wilaya hizo kuwa ni Rombo, Mwanga, Same na Siha.

Amesema kuwa magari hayo 20 ya aina mbalimbali yakiwamo malori saba, yana thamani ya shilingi za Kenya 80,860,000 sawa na fedha za Tanzania Sh1.7 bilioni.

Aidha, miongoni mwa magari hayo ni Toyota Landcruiser manne, Mercedes Benz tatu, Mercedes Benz truck (lori), Toyota prado moja, Toyota Probox moja, Toyota axio moja, Toyota Allion moja, Toyota Mitsubish nne na Nissan Patrol V.8 Station wagon.

“Hatua hiyo imekuja kutokana na kuwepo kwa wimbi la wizi wa magari yanayoibiwa nchini Kenya yanayopitia mkoa wa Kilimanjaro na baadaye kwenda mikoa mingine,” amesema kamanda Issah

Aidha, amesema kuwa watuhumiwa tisa wanashikiliwa wakihusishwa na magari hayo ambapo, Polisi Kilimanjaro kwa kushirikiana na polisi wa Dar Es Salaam walifanikiwa kuubaini mtandao huo ambapo tayari watu tisa wamekamatwa jijini Dar es salaam.

 

Van Dijk ang'ara tuzo za mwanasoka bora Ulaya
JPM atoa wito kwa viongozi wa Kiafrika, 'Jiepusheni na fikra za kikoloni'