Bodi ya Nyama Tanzania imesema kuwa ifikapo Septemba 30, 2019 itakuwa mwisho kwa wauza nyama mabuchani kutumia magogo na endapo mtu atakaidi, hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.

Hayo yamesemwa jijini Dar es salaam na Ofisa Usajili kutoka katika bodi hiyo, Geofrey Sosthenes katika maonyesho ya biashara ya kimataifa yanayofanyika katika viwanja vya Sabasaba.

Amesema kuwa magogo hayo pia yanasababisha hasara ya upotevu wa nyama, kitaalamu katika kilo 100 inapotea kilo moja, ambapo kwa mwaka muuzaji hupoteza Sh. milioni 3.8 ambayo inatosha kununua machine ya kisasa ya kukatia nyama.

Aidha, ameongeza kuwa watakao kaidi agizo hilo watachukuliwa hatua na Msajili wa bodi hiyo, kwa sababu tayari amekwisha ziandikia barua mamlaka za Serikali za Mitaa tangu Februari mwaka huu kuwataka wakurugenzi wa idara zote kuhakikisha wanaboresha maeneo yote yanayozalisha nyama ikiwa ni pamoja na machinjio na mabucha.

“Kama una bucha inauza kilo 200 kwa siku unaona ni kiasi gani unapoteza, ukipiga hesabu yako kwa mwaka unapoteza sh. milioni 3.8 ambayo inatosha kununua mashine ya kisasa ya kukatia nyama, tunawasihi kuacha kuyatumia magogo kwa sababu si salama kwa afya za watumiaji,” amesema Sosthenes

Hata hivyo, ofisa huyo amesema kuwa watahakikisha wanawashauri wamiliki wa mabucha kuhakikisha wanakuwa na mabucha ya viwango ambayo yapo kwenye sheria, viwango hivyo ni pamoja na kuacha kutumia magogo hayo, jambo ambalo wamekwisha lisisitiza.

 

Lugola aapa kula sahani moja na Polisi wasiokuwa waaminifu
Mnatakiwa kujivunia miradi inayotekelezwa na serikali- Omary Mgumba