Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, dkt. John Pombe Magufuli tarehe 28 Februari, 2020 amekagua maendeleo ya ujenzi wa Msikiti mkubwa wa baraza Kuu la waislamu tanzania (BAKWATA) unaojengwa Kinondoni Jijini Dar es Salaam.

Sheikh Mkuu Aboubakar Zubeir bin Ally ameongoza Dua ya kumuombea Rais na kuliombea taifa ili Mwenyezi Mungu aiepushe Tanzania dhidi ya maradhi ya homa ya virusi vya corona, kudumisha amani na utulivu na kuombea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika baadaye mwaka huu ufanyike vizuri na kwa amani.

Akiongozwa na Mufti wa Tanzania, Sheikh Aboubakar Zubeir bin Ally, Magufuli amejionea kazi za ukamilishaji wa jengo jipya la Msikiti na jengo la ofisi ya Taasisi ya Mfalme Mohammed VI wa Morocco zikiendelea kukamilishwa, na ameelezea kufurahishwa kwake na ubora na uzuri wa Msikiti huo.

Msikiti huo unajengwa kwa ufadhili wa Mfalme Mohammed VI wa Morocco baada ya kuombwa na Rais Magufuli alipofanya ziara rasmi hapa nchini Oktoba 2016.

Mhe. Rais Magufuli amemshukuru Mfalme Mohammed VI wa Morocco kwa kutekeleza ombi alilomuomba la kuwajengea waislamu msikiti mkubwa kuliko yote hapa nchini.

Mufti wa Tanzania, Sheikh Aboubakar Zubeir bin Ally amemshukuru Rais kwa kuwajali Waislamu na kuwaombea msaada wa kujengewa Msikiti huo ambao ujenzi wake umefikia asilimia 97.

Msekwa achambua Membe kufukuzwa CCM, ‘hata kama ni uamuzi wa kunyongwa’
Membe atoa kauli ya kwanza baada ya kufukuzwa CCM