Rais John Magufuli ameingilia kati sakata la uhaba wa sukari unaoanza kujitokeza nchini na kupelekea kufumuka kwa bei ya bidhaa hiyo ikiwa ni siku chache tangu apige marufuku utoaji holela wa vibali vya kuagiza nje bidhaa hiyo.
Akiongea na wananchi wa Kateshi, Mkoani Manyara jana, Rais Magufuli aliwaonya wafanyabiashara wanaoficha tani za sukari ili kusubiri ongezeko la bei.
Rais ameviagiza vyombo vya dola kufuatilia kwa ukaribu na kukamata sukari hiyo inayofichwa na wafanyabiashara hao huku akiahidi kuigawa sukari hiyo bure kwa wananchi.
Alisema kuwa tayari anazo taarifa za wafanyabishara wawili walioficha sukari, mmoja akiwa amenunua tani 3000, Kilombero na kwamba hataki kuzichukua makusudi, huku mwingine akiwa ameficha tani 4000 katika magodauni yaliyoko Mbagala jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo, Rais aliwatoa hofu wananchi akieleza kuwa Serikali iko katika hatua za kuagiza sukari ya kutosha nje ya nchi ili kukabiliana na wafanyabiashara hao wasiotumia njia halali kuagiza sukari nchini Brazil.