Mahakama Kuu ya Tanzania, imetoa wito kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai na Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe kufika mahakamani hapo leo, kesi ya Kikatiba kuhusu madaraka ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) itakapotajwa.

Zitto akishirikiana na mwanasheria wake, Fatma Karume alifungua kesi hiyo iliyosajiliwa kwa namba 01/2019, akiiomba Mahakama kutoa tafsiri ya Ibara ya 143(6) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alifungua kesi hiyo akipinga hatua ya Spika Ndugai kumuita CAG, Profesa Mussa Assad ili ahojiwe na Kamati ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge kuhusu kauli yake aliyoitoa akiwa nchini Marekani katika mahojiano na chombo cha habari cha Umoja wa Mataifa, kuwa “kama Bunge halifanyii kazi ripoti zangu, huo ni udhaifu wa Bunge.”

Januari 21, CAG aliitikia wito wa Spika Ndugai na kuhojiwa na Kamati hiyo ya Bunge ambayo ilisema kuwa utaratibu mwingine unaendelea baada ya mahojiano hayo.

Kesi hiyo inatajwa leo huku ikiwa imepangiwa jopo la majaji watatu, Jaji Firmin Matogolo, Dkt. Benhajj Masoud na Elinaza Luvanda.

Klopp aitupia lawama ‘theluji’ kukosa pointi 3 jana
Askari Polisi aponzwa na matokeo ya kidato cha nne