Mahakama Kuu ya Tanzania, leo imekataa kupokea kesi ya kikatiba iliyofunguliwa na Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe na wenzake kuhusu uamuzi wa Spika wa Bunge, Job Ndugai kumuita kwenye Kamati ya Bunge, Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad.

Barua ya kukataa kuisajili kesi hiyo, imetolewa na msajili msaidizi wa Mahakama Kuu, S.S Sarwatt ikitoa sababu kuu mbili za kisheria.

Sababu hizo ni pamoja na kutoambatishwa hati za viapo za baadhi ya walalamikaji katika kesi hiyo pamoja na nakala ya wito au amri ya Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kumuita CAG.

“Wito au amri inayodaiwa kuwa imetolewa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano pamoja na hati ya kiapo ya CAG havikuambatishwa kwenye maombi haya,” imeeleza barua hiyo.

Kufuatia hatua hiyo, Zitto akiongozwa na wakili Fatma Karume wameonesha kushangazwa na sababu zilizotolewa na Msajili Msaidizi wakidai kuwa anachokiomba ni ushahidi ambao unapaswa kuwasilishwa Mahakamani na sio kwenye hatua ya usajili.

Kufuatia sakata hilo, Jaji Mkuu wa Tanzania amemuandikia barua Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu akimtaka ashughulikie suala hilo la kukataliwa kusajiliwa kwa kesi hiyo.

Video: Wakili msomi awapa darasa wanasiasa,'Msiukimbie Muswada'
Video: Mnyama mwenye wivu zaidi duniani