Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameyaomba mashirika ya Kimataifa na Nchi zilizoendelea zishirikiane na Serikali ya Tanzania katika kuwahudumia wakimbizi.

Waziri Mkuu Majaliwa ameyasema hayo leo  Juni 6, 2016alipofanya mazungumzo na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Ubelgiji, Mhe. Dibr Reynders ofisini kwake Bungeni, Dodoma.

“Kwa sasa tunashirikiana na UN (Umoja wa Mataifa) kuwahudumia wakimbizi, hivyo tunaomba mataifa mengine nayo yatusupport  katika jambo hili,” amesema.

Amesema Tanzania  inahifadhi jumla ya wakimbizi 165,000 kati ya 230,000 walioko katika nchi za Maziwa Makuu, ambapo bajeti ya Serikali haitoshelezi kuwapa huduma wanazostahili.

Waziri Mkuu Majaliwa amesema wakimbizi hao wanaishi kwenye kambi mbalimbali nchini zikiwemo za Nyarugusu na Nduta zilizoko wilayani Kasulu na Kibondo ambazo alizitembelea Desemba mwaka jana.

Amesema wakimbizi hao wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo za uhaba wa maji safi, ufinyu wa huduma za afya na elimu na uharibifu wa mazingira .

Amesema wengi wa wakimbizi hao ni raia wa Burundi, Kongo na Rwanda, pia amemuomba Mhe. Reynders atakapofika Burundi akahamasishe amani.

Pia Waziri Mkuu Majaliwa amesema Tanzania inakkaribisha wawekezaji kutoka nchini Ubelgiji na mataifa mengine kuja kuwekeza katika Sekta za Viwanda, Nishati na Miundombinu.

Aidha Waziri Mkuu Majaliwa amesema hali ya siasa visiwani Zanzibar ni ya utulivu na Rais Dk. Ali Mohamed Shein anafanya kazi vizuri kwa kushirikiana na vyama vya upinzani.

Waziri Mkuu Majaliwa ameyasema hayo wakati akijibu swali la Mhe. Reynders aliyetaka kujua hali ya kisiasa inavyoendelea visiwani huko.

Wahamiaji haramu 1976 warudishwa nchini kwao.
Lowassa: Ninasononeshwa na hali ya Watanzania hivi sasa