Ndoto ya kimyakimya ni mahala pazuri zaidi pa kuificha siri kwakuwa wakati mwingine hata wewe mwenyewe unapojaribu kuikumbuka inaweza kukupotea, au hata ukaikumbuka na usielewe ilikuwa na maana gani!

Hayo ni sehemu ya maisha ya kisiasa ya mwanasiasa nguli, inaaminika ni mjuzi wa masuala ya kiintelijensia, Mwanadiplomasia na Waziri wa Mambo ya Nje wa Serikali ya Awamu ya Nne, Bernard Membe, ambaye hivi sasa anachekelea ingawa yuko kwenye kibano kikali akipita kwenye ncha ya wembe.

Kigogo huyu huishi kwa mafumbo yaliyojaa ‘siri’ ambayo naamini ndiyo silaha yake kuu, ukiweza kufumbua mafumbo yake basi umempata!

Kwa mnaokumbuka vizuri, mwaka 2014, wakati wa vuguvugu la nani atagombea urais mwaka 2015 kupitia CCM, Membe aliyekuwa miongoni mwa watu watatu wenye nguvu kubwa wakati huo, lakini hakuwahi kutoa jibu la uamuzi wake akieleza kuwa anasubiri ‘aoteshwe’. Aliamini siri ya urais iko kwenye ndoto, akasubiri aoteshwe. Na aliamini siku atakapooteshwa tu atachukua fomu mara moja.

Je, wewe umewahi kutamani kuota nini? Achana na ndoto nyevu za wavulana, nazungumzia ndoto ya mafanikio. Wengi wakiota wanaendelea kulala kwakuwa ndoto tamu hawataki kuamka. Hiyo sio ‘type’ ya mzee Membe.

Hata hivyo, kama nilivyoeleza kuwa maisha yake yamejaa mafumbo na siri, labda kutokana na ile tunayosadiki kuwa amekuwa mtu wa ‘kiintelijensia’, Membe aliweka wazi kuwa haikuwa ndoto ile ya kawaida ya kuamka umechana mashuka baada ya kuota ulikuwa unavuna mikonge.  Ndoto kwake lilikuwa fumbo, japo sio fumbo la imani.

“Kusubiri kuoteshwa namaanisha ni pale wenzako watakaposema kwamba tumekupima na kwamba tumeona unaweza. Hapo ndipo unapoweza kuja kusema nadhani ile ndoto imetimia,” Membe alijibu swali la waandishi wa habari wa gazeti la Mwananchi, Septemba 2014.

Alifumbua fumbo la ndoto yake aliyoisubiri ili achukue hatua. Ingawa hakutangaza kuwa ameoteshwa tayari, vitendo vilizungumza zaidi. Miezi saba baadaye aliingia kwenye kinyang’anyiro kuusaka urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akishiriki kwanza mchakato kwenye chama chake.

Kishindo cha ukimya, siri na mafumbo ya Membe kilitikisa ardhi ya kisiasa ya chama hicho. Alikuwa na timu kubwa yenye misuli ya kuogofya wapinzani wake, ‘Timu Membe’. Lakini kwa kipimo cha macho, mpinzani wake mkuu mwenye misuli na sifa zinazoshabihiana naye alikuwa Edward Lowassa, Waziri Mkuu wa zamani. Hawa wote walikuwa moto. Hawa wote waliishi kwa mafumbo na siri, lakini walipotoka mafichoni ilikuwa ‘ilikuwa kama kukutana na ‘upepo wa kisulisuli’, maana walisomba watu kila kona wakatengeneza mafuriko ya watu.

Bernard Membe akimsalimia, Edward Lowassa kwenye kikao cha Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi

Lakini kwa bahati mbaya walijisahau kuwa wao wameshika makali na mpini umeshikwa na Kamati Kuu na Halmashauri Kuu na Kamati Kuu ya chama hicho, na wakati huo Kamati ilikuwa imeongeza makali. Wote ‘walikatwa’ kwa mitindo tofauti; na safari yao ya urais ndani ya CCM ikaishia hapo. Wembe wa CCM unakata, na ni uleule…. alisema Marehemu Kaptain Komba.

Au ndio tuseme wakati ule Membe hakuielewa vizuri tafsiri ya ile ‘ndoto aliyooteshwa’?

Baada ya uamuzi huo, kila mmoja alibaki na siri yake moyoni kuhusu hatua zaidi atazochukua. Alianza Lowasa ambaye licha ya kuapa kubaki ndani ya CCM, alikuwa na yake moyoni. Siri ilikaa ndani ya siri, kumbe anataka kuhamia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo. Lakini hata picha ziliposambaa akionekana kutoka kwenye mkutano wa Kamati kuu ya Chadema, hata Chadema wenyewe walikana. Ilikuwa siri.

Ndiyo, hata mimi ningewashauri waangalie kwanza upepo waifanye siri, kwa sababu tangu mwaka 2008 walikuwa bize wakimrushia tope Lowassa kwa kashfa nzito, miaka saba baadaye wanampa bender ana silaha awaongoze vitani kama shujaa!!! Kwakweli siasa ni mazingaombwe ya kisayansi. Hata baadhi ya watumishi wa Mungu wamewahi kupotea walipojaribu kutabiri masuala ya kisiasa. Waachieni akina Kaisari mambo yao wanajuana! Waliamini hiyo siri ndiyo silaha yao, lakini kilichofuata ni historia tu. Palichimbika sana lakini….! Tuyaache ya Mzee Lowassa na historia aliyoiandika, Wapinzani hawatamsahau ingawa sasa amerudi nyumbani kwao.

Ndugu yetu, mzee wa mafumbo, yeye aliingia kwenye mapambano, hakuacha gwanda lake la kijani, akamuunga mkono mgombea aliyechaguliwa, Dkt. John Pombe Magufuli. Alizunguka, akapanda kwenye majukwaa kadhaa akimnadi, alijibu hoja kadhaa kukitetea chama na kuonesha ‘tuko pamoja’.

Lakini baada ya Dkt. Magufuli kushinda na kuapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na baadaye kuwa Mwenyekiti wa CCM-Taifa, Membe alienda likizo. Hakuwahi kuonekana tena kwenye shughuli za chama. Na siku alipoonekana hadharani alidai ‘yeye ni yatima na ni mmoja ya waliokatwa mkia’. Siku hiyo ile meme ya Dkt. Shika anasema ‘tutaelewana tu, ngoja kwanza tuoneshane makali kidogokidogo’ ilishika kasi mitandaoni.

Sasa usiri, ukimya wake ‘haukuchukuliwa poa’ na CCM. Wajuzi wa mambo huwa hatukubali kumuacha kobe ainame atunge sheria. Tunajua akikamilisha mchakato wake hatujui nini kitafuata!

Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Bashiru Ally ni mmoja wa wajuzi hao, alishindwa kuvumilia, akaona ni bora kumuinua kobe asiendelee kutunga sheria. Yule shabiki wa Yanga mzee wa kigelegele anasema ‘potelea pwete, liwalo na liwe’.

Desemba mwaka jana, akiwa kwenye kikao cha ndani Mjini Geita, Dkt. Bashiru akarusha kombora, akamtaka Membe ajitokeze na afike ofisini kwake ili azungumze naye na ajibu maswali yanayoulizwa. Swali kuu ilikuwa imelenga ukimya wake. Dkt. Bashiru anajua ukimya wa Membe huku kukiwa na minong’ono fulani sio wa kuukalia kimya, huyu ni yule jamaa wa mafumbo, siri na ndoto, asije kuota mengine akaanza kuvuruga mambo. Akamtaka ajisalimishe ofisini.

Sasa, utauliza ilikuwa minong’ono ipii! Komredi Membe alianza kutajwatajwa kwenye mitandao ya kijamii, ikielezwa kuwa ameanza ‘figisu’ za chini kwa chini akitafuta kuungwa mkono ndani ya CCM. Wengine walidai, ‘Jamaa yetu ameanza kuota tena zile ndoto zake za mwaka 2014, na kipindi hiki anataka kupita njia za panya, eti sasa hivi ni zaidi kwa sababu ana ‘connection’ nyingi!’. Mitandao bana, hata ukitaka kuota inajua unataka kuota nini!

Lakini Membe aliukataa utaratibu wa wito wa Dkt. Bashiru, akadai “CCM kuna utaratibu wa kuitana.” Huyu Membe anaijua vyema Katiba ya chama chake bana! Si unajua tena alikuwa anajiandaa kuwa Mwenyekiti wa chama Taifa, sasa si inabidi ujisomee muongozo, wazungu wanasema ‘just in case…!’

Minong’ono hiyo iliibua watu wengine, wakaanza kumuanika. Lakini, kumbuka nilikwambia Membe ni mkali wa mafumbo na siri kali! Lakini sio mvumilivu kama Lowassa, ukimgusa hawezi kukuacha upite hivihivi.

Katika sakata la kumuanika yeye na kilichoitwa ‘siri na njama zake’, aliguswa na Cyprian Musiba. Membe aliamua kuingia vitani, ukija na manati yeye anakuja na kifaru kabisa, akampeleka Musiba Mahakamani akimshitaki kwa kumchafua. Wenzake akina mzee Yusuf Makamba na Abdulrahman Kinana wao waliandika waraka wakayatoa waliyoamini ni ya moyoni kuhusu Musiba na mengine. Wakayazua ya kuzua, lakini baada yah apo wakasema baasi tushafunguka’. Lakini Membe yeye alisema hakuna haja ya kuandika ngonjera wakati umeshapakwa tope wakati unawaza ndoto inakuja lini, akaamua kwenda naye kisheria hadi mwisho. Akamburuza mahakamani na anahudhuria kesi hiyo mwenyewe ngazi kwa ngazi.

Desemba, 2017 mfanyabiashara aliyewahi kuwa Mbunge wa Igunga na Mwanasiasa kigogo aliyestaafu siasa, Rostam Aziz alimrushia kombora zito Membe, akimshauri kuachana na ndoto za kuchukua fomu ya kuomba kupitishwa na chama hicho kugombea urais 2020, ili kuenzi utamaduni wa chama hicho wa miaka 10 ya urais.

Kama ilivyo kawaida, mzee wa mafumbo, alikuwa kimya kwa muda hadi Mei 18, 2018 akiwa nje ya Mahakama ya Kisutu jijini Dar es Salaam akifuatilia kesi yake dhidi ya Musiba. Alimjibu Rostam kwa mafumbo na maneno dhahiri.

“Rostam asijaribu kuwa more Christian than the Romans (asijaribu kuwa mkristo bora zaidi ya Waroma, nadhani mtanielewa,” alisema Membe. Hapo naamini umelifumbua hilo.

Akaongeza, “Rostam wewe ni mwenzetu sisi tumekatwa mikia, ukikatwa mkia hata ukijitahidije mkia wako ni mfupi tu… Rostam ni mchumi mzuri sana kwenye masuala ya uchumi, tuzungumzie masuala ya uchumi wa nchi yetu, haya yatampa heshima kubwa kuliko kujaribu kuwa ‘mtoto mzawa’ badala ya kukubali status ya kwamba Rostam na mimi ni watoto wa kambo.”

Sasa utakubaliana nami kuwa inabidi uwe mzuri kwenye kutegua vitendawili na kufumbua mafumbo ili umuelewe vizuri Komredi Membe, la sivyo utawaza mikia ya ng’ombe na ubora wa ukristo, mwisho yatakuchanganya tu.

Turudi kwenye mtiririko wa safari ya kuelekea kuwekwa kitimoto na jeuri/ujasiri yake:

Kwa bahati (wewe utasema nzuri au mbaya), teknolojia ikavumisha moja kati ya siri za Komredi Membe. Marehemu Ruge Mutahaba, Jasiri muongoza njia aliwahi kusema, “dunia ya leo muogope Mungu na teknolojia’. Mara paap! Sauti za mazungumzo ya siri ya simu kati ya Membe na rafiki zake kuhusu viongozi wa CCM ikavuja. Ikawa shida, jamaa alikuwa anatema cheche zake akijua yuko faragha, ghafla ikawashwa taa mambo yote hadharani. Kwenye simu ile hakukuwa na mafumbo, hapo alitiririka tu mambo dhahiri shahiri.

Ingawa wakati sauti yake inavuja, sauti za makada wengine waandamizi na waliokuwa viongozi (Abdulrahman Kinana na Yusuf Makamba – Makatibu wakuu wastaafu wa CCM, Nape Nnauye, Januari Makamba na William Ngeleja) nazo ziliingia kwenye mitandao. Nape, Januari na Ngeleja wao wakaomba msamaha wakasamehewa. Mzee Makamba na Komredi Kinana wao wakaa kimya.

Lakini Membe kwa uaminifu akakiri tu kuwa sauti zile ni za kwake, huku akimlaumu aliyezisambaza kwani ilikuwa faragha yake. Alisema tatizo sio sauti, zile ni sauti zake lakini tatizo ni aliyezisambaza kwakuwa ni faragha yake.

Kutokana na hilo na yale mengine, Kamati Kuu ya CCM iliyokutana Desemba mwaka jana, ikaamua Membe, Kinana na Makamba wahojiwe na Kamati ya Maadili/Nidhamu na Usalama. Kamati hiyo ilitekeleza maagizo na kuipanga Februari 6, 2020 kuwa siku husika.

Kilichotushangaza wengi, ni hatua ya Membe kueleza kuwa alikuwa anaisubiri kwa hamu siku hii, tofauti na wengi tulivyokuwa tunadhani huenda angesema, ‘ikiwezekana kikombe hiki kiniepuke’.

Kwa waliosoma kwenye akaunti ya Twitter ambayo imekuwa ikitoa kauli za Membe na yeye hajawahi kuikana, pamoja na mahojiano aliyofanya na Azam TV, tulijiuliza anafurahia nini wakati anahojiwa kwa tuhuma nzito na walioshika mpini wanaweza kufanya lolote, yeye ameshika makali? Ina maana Membe amesahau kuwa kamati huwa ‘inakata’?

Tabasamu la Membe kwenye ‘kibano’ linatoka wapi?

Baada ya Kamati ya Maadili ya Chama Cha Mapinduzi kumuita rasmi Membe kwa ajili ya kumhoji, kwanza alitangaza yeye mwenyewe kupitia Twitter, na tangazo lake lilikuwa la furaha. Kabla hajaanza safari kwenda jijini Dodoma kuwekwa kitimoto, alieleza kuwa alikuwa anaisubiri sana siku hiyo.

Tukajiuliza ameupata wapi huu ujasiri wakati tunajua hata Bungeni ukiitwa kwenye Kamati ya Maadili lazima kijasho kikutoke, kwa sababu lolote linaweza kutokea, kamati imeshika mpini wewe umeshika makali.

Ujasiri wa Membe na furaha yake naamini ilitokana na mambo yafuatayo:

Kwanza, Membe ni moja kati ya nguli ndani ya chama, ingawa hakuwa kwenye nafasi za juu sana za uongozi awali, lakini tangu 2007 alikuwa Mjumbe wa Kamati kuu ya chama. Ndani ya Serikali alikuwa anacheza nafasi nyeti na muhimu sana.

Wahenga wa Kijamaica wanasema “a new broom sweeps clean, but the old one knows all the corners”. Kwa tafsiri isiyo rasmi, “fagio jipya hufagia vizuri lakini fagio la kale (zee) huzijua kona zote.”

Kwa tuliomfahamu sana Membe baada ya kuoteshwa mwaka 2014 na kuchukua hatua mwaka 2015, tukumbushane tu kuwa huyu aliwahi kuwa mchakataji wa taarifa za kiusalama kwenye Ofisi ya Rais kwa kipindi cha miaka 11 (1978 – 1989).

Lakini pia, Mzee Membe ni mtaalam wa siasa, sio za kipaji au wito. Yeye amesomea Sayansi ya Siasa katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Kuhusu kukaa kwenye vikao vya kitimoto, iwe ni kusuluhisha au ku-negotiate masuala makubwa yaliyoharibika, amefanya kwa ngazi za kimataifa; na amesomea mahusiano ya kimataifa katika Chuo Kikuu cha John Hopkins kilichoko Maryland, Mashariki mwa Marekani. Alipomaliza tu masomo yake mwaka 1992 alipewa kazi ya kuwa mshauri wa Ubalozi wa Tanzania nchini Canada. Ubunge, Unaibu Waziri na hatimaye Uwaziri ameanza mwaka 2000 baada ya wana Mtama kumchagua kuwa Mbunge wao.

Unaukumbuka ujasiri wa Membe? Chini ya Rais Jakaya Kikwete alisimama akaitangazia dunia akilaani vikali vitendo vya Israel kuishambulia Palestina kwenye ukanda wa Gaza, mwaka 2010. Akiwa kama Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Aliwachana Waisrael, akawaambia waache kutumia bunduki na mabomu dhidi ya Wapalestina wanaotumia mawe na manati. Akaitaka pia kuvunja ukuta unaowatenganisha. Ilikuwa siku ya Umoja wa Mataifa ya kuungana na Wapalestina.

Bernard Membe (akiwa Waziri wa Mambo ya Nje) akimuonesha kitu Hillary Clinton (akiwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani) baada ya kumpokea katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Juni 11, 2011

Wanasaikolojia wanasema ukiwa unadhani uelewa sana wa kitu fulani kwanza inapunguza uoga na pili hata ukiwa kwenye hatari wakati mwingine ‘haikushtui’. Kwa sababu unaweza kuzubaishwa na uelewa wako.

Lakini kuna hatari sana ya kuwa ‘mjuaji kupita kiasi’. Mwandishi nguli wa Marekani, George Horace Lorimer anasema, “kama kuna kitu kibaya zaidi ya kuwa na uwelewa mdogo, ni kuwa na uelewa uliopita kiasi. Elimu itapanua akili ndogo, lakini kumbuka hakuna dawa ya kuvimba kichwa, kwa sababu mwisho kitapasuka tu.”

Pili, huyu Komredi Membe alikuwa na silaha yake moja nzito, ambayo ni siri ambazo aliamini hata wanakamati hawazijui na amepanga kwenda kuitumia. “Nitawaambia wanayoyajua na wasiyoyajua,” alisema Membe kwa furaha na bashasha kwenye mahojiano na Azam TV. Anaamini Kamati kuna mambo hawayajui, wakati huu nadhani aliamua hatatumia mafumbo tena, atafungua makablasha yote awape siri zote. Aliamini wakiyajua watamuelewa.

Labda ndio maana aliwahi kufika mbele ya Kamati hiyo, na baada ya kumaliza kuhojiwa akasema ilikuwa siku nzuri sana kwake kiasi kwamba anaenda kusherehekea na mkewe kwa kupata msosi wa nguvu kwenye hoteli moja nzuri, kabla hawajarejea jijini Dar es Salaam.

Membe wa Twitter aliandika, “Namshukuru Mungu kwa ujasiri alionipa wa kwenda mbele ya Kamati ya maadili na nidhamu na kujibu hoja mbalimbali bila woga, bila kuyumba wala kuyumbishwa! Naamini wameupokea ushauri niliyoutoa kuhusu Uhuru, Haki, Uchaguzi na Uhusiano wa kimataifa.”

Hayo ni ya Membe, tunasubiri Ripoti Rasmi ya Kamati ambayo itawasilishwa kwenye Kamati Kuu ya chama hicho tawala, ukiwa ni mwaka wenye joto la uchaguzi. Majibu rasmi huenda yakapatikana ndani ya kipindi cha siku 45. Tuwe na subiria.

Lakini kabla sijamaliza, nikukumbushe tu, kwenye siasa huwa hata kama umefanya mambo gani makubwa, kuna wakati ukitereza moja huwa linakuwa anguko lako kuu. Mzee Jakaya Kikwete, Rais Mstaafu anaita ‘ajali ya kisiasa’. Hiyo ajali iliwahi kumpata rafiki yake, Edward Lowassa, alipolazimika kujiuzulu Uwaziri Mkuu.

Mfano, Rais wa 37 wa Marekani, Richard Nixon yeye alifanya makubwa sana, alikuwa Rais wa kwana wa Marekani kutembelea Jamhuri ya watu wa China na kuleta amani, alifanikiwa kuyaondoa majeshi ya Marekani nchini Vietnam, alianzisha mazungumzo ya amani na Umoja wa Kisoviet.

Lakini mbali na uzuri na umashuhuri wake wote, aliangushwa kwa kishindo na kupakwa tope zito lililofuta kila kitu, baada ya kubainika kuhusika kwenye sakata maarufu la ‘Watergate’. Alilazimika kuachia madaraka, akatoka White House akiwa na doa moja zito lililochafua usafi wa nguo zake zote. Ni baada ya kubainika kuwa baadhi ya maafisa wa ikulu walikuwa kati ya watu watano waliojaribu kuvamia Ofisi za Makao Makuu ya chama cha upinzani zilizokuwa kwenye jengo la ‘Watergate’ jijini Washington DC. Walikamatwa, Serikali ilijitahidi kuficha utambulisho wao lakini waandishi wa habari za kiuchunguzi walimwaga mchele, wakawaanika, ikawa balaa. Ilikuwa Juni 17, 1972. Nenda ukasome kidogo, uone filamu ya siasa ilivyo tamu.

Eee bana eeeh, ya Ngoswe tumuachie Ngoswe, sisi tujadili yetu hapa. Huo ulikuwa mfano tu, na kwa leo naishia hapo. Siasa ni bahari kuna wakati inakuwa tulivu ya kushawishi ukapunge upepo na kuvinjali, lakini usisahau kuna wakati wa Tsunami.

Tusubiri tuone, maana mwaka 2015 ulikuwa na matukio ya miaka 10, mwaka huu itakuwaje? Nikki wa Pili mtoto wa mzee Simon, kwenye wimbo wake wa ‘Good Boy’ alisema, “hakuna aijuae kesho hata mtunzi wa kalenda.” Tusishangae Membe akawa Mpeperusha bendera wa ACT-Wazalendo au Chadema, ‘who knows’! 

Lakini Membe akumbuke kale ka wimbo kazuri ka Marehemu Kapten John Komba, “kwa CCM, Wembe ni uleule…”

Video: Aliyechana Quran asimamishwa kazi, Membe atamba kuipa darasa kamati ya maadili CCM
Atupwa jela kwa kujaribu kujiua