Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda ameahidi kuwasomesha wanafunzi wakike 100 waliofaulu kidato cha nne mchepuo wa sayansi katika mkoa huo kuanzia kidato cha tano hadi chasita “Advanced level”, ili kuhakikisha wanawake hawaachwi nyuma katika suala la maendeleo ya sayansi na Teknolojia.

Ametoa ahadi hiyo katika maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani ambayo hufanyika kila mwaka tarehe 8 mwezi wa 3, ambapo kwa mkoa wa Dar es salaam wanawake kutoka taasisi mbalimbali na vikundi wamekutana Mlimani city, Makonda akiwa mgeni rasmi.

Amesema kuwa watoto wakike wanapitia changamoto nyingi katika suala la kupata elimu ambayo ndiyo mkombozi wa wanawake hivyo nilazima watoto hao wapewe nafasi ya upendeleo katika kuhakikisha wanapata elimu bora na kuhakikisha hilo yeye anaanza kwa kuwasomesha wanafunzi wakike 100 katika mkoa wake bure.

Aidha, katika hatua nyingine amesema kuwa licha ya serikali kuendelea kuboresha huduma za Afya na maji kwa wanawake hasa kuhakikisha wanapata huduma hizo kwa ukaribu, amefanikisha kukamilisha utafiti wa wanaume wanaotelekeza watoto ambao mwisho wa mwezi huu atawasilisha kwa waziri mwenye dhamana ili kusaidia kurekebisha sheria itakayowabana wanaume wanaokwepa majukumu ya kulea watoto.

“Wanaume wanaotelekeza watoto wajiandae kupata chamtema kuni, sheria mpya inakuja siyo ile ya kulipa, nataka wanaume kabla hawajazalisha wawe wanajifikiria kwanza kama wana uwezo wa kulea,”amesema Makonda.

Aidha, ametoa wito kwa wanawake kuhakikisha wanakuwa kipaumbele cha kumiliki ardhi na kushiriki katika uchaguzi ngazi za ugombea ili kuenda sambamba na kauli mbiu ya mwaka huu “Badili fikra kufikia usawa wa kijinsia kwa maendeleo endelevu”

Boomplay yawapa shavu wasanii maarufu wa kike
Video: Wanawake wahimizwa kufanya kazi za Tehama