Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amewataka wananchi kwa ujumla kuendelea kuwa watulivu kwakuwa vyombo vya ulinzi na usalama vipo kazini na kwamba ana imani msanii Roma na wenzake waliotekwa watapatikana kabla ya Jumapili.

Mkuu huyo wa Mkoa alitoa ahadi hiyo jana baada ya wasanii wakiongozana na mke wa Roma, Bi. Nancy kumtembelea mkuu huyo wa mkoa kwa lengo la kumuomba awasaidie kuwapata ndugu zao.

“Nawapa imani, haitafika Jumapili tutakuwa tumewapata ndugu zetu wote wanne. Na mimi naomba kwa dini zetu, kwa imani zetu, kila mmoja popote alipo aombe ili tuhakikishe ndugu zetu hawa tunawarejesha wakiwa salama,” alisema Makonda.

“Tunazo nyenzo nyingi na mbinu mbalimbali ambazo zitatusaidia kuwapata. Moja kubwa ambalo libaki kwenye fikra za watu, hakuna serikali inayoweza kufumbia macho kupotea kwa watu wake hata siku moja. Tunaowajibu wa kulinda uhai hata wa mtu mmoja,” aliongeza.

Aidha, Mkuu huyo wa mkoa ambaye pia ni Mwenyekiti waKamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Dar es Salaam aliwataka wananchi kutoa taarifa zozote sahihi za kusaidia vyombo vya usalama kufanikisha zoezi hilo muhimu na nyeti.

Aliwatoa hofu wananchi wa mkoa huo kuwa suala la utekaji na ujambazi litadhibitiwa vikali na Serikali na kwamba hakuna mwananchi atakayepotea bila kuwa na majibu ya kilichotokea dhidi yake.

DC Mjema apiga marufuku shughuli za uchimbaji kokoto eneo la Pugu
Young Killer afunguka mazungumzo yake na Diamond 'kufanya kazi'