Maktaba ya chuo kikuu nchini Zambia imepiga marufuku wanafunzi wa kike kuingia ndani ya jengo hilo wakiwa wamevaa vimini kwakuwa wanawachanganya wanafunzi wa kiume wakiwa wanasoma.

Chuo Kikuu cha Zambia iliyopo katika jiji la Lusaka imeweka tangazo maalum kuzunguka maktaba yake hiyo kubwa kuwataka wanafunzi wa kike kuvaa mavazi ya heshima.

Wanafunzi wa chuo hicho chenye jina kubwa barani Afrika wanasifika kwa kuvalia mavazi ‘yanayokwenda na wakati’, wakichukua mitindo ya watu maarufu zaidi kwenye ulimwengu wa muziki na uigizaji.

“Tumebaini kuwa wanafunzi wengi wa kike wanaingia maktaba wakiwa wamevaa nusu uchi, hali inayowachanganya wanafunzi wa kiume,” tangazo hilo limeeleza.

“Kwahiyo, tunawataka wanafunzi wa kike kuvaa mavazi ya heshima wanapokuwa wanatumia maktaba. Mavazi ya heshima ndio njia ya kwenda nayo,” linasomeka zaidi tangazo hilo.

Hata hivyo, tangazo hilo limepata mapingamizi kutoka kwa wanafunzi wa kike ambao wamedai wanafunzi wa kiume hawawezi kuchanganywa na miguu kama wameamua kwenda kusoma.

“Kama mpango wako ni kwenda maktaba kusoma, kwanin unaanza kuacha kilichokupeleka na kuangalia vitu kama miguu ya wanawake? amehoji Dikina Muzeya alipozungumza na BBC.

Aidha, wanafunzi wa kiume kwa wingi wao wameonesha kuunga mkono tangazo hilo wakidai kuwa kutokana na namna ambavyo miili ya wanawake imeumbwa kuwa ya mvuto, ni vigumu sana kuacha kuwaangalia wanapokuwa wamevaa vimini.

 

Mamlaka yamsaka chui aliyekula mtoto wa miaka mitatu
Mnasema elimu imeshuka wakati Panya wanafundishwa na wanaelewa?- JPM