Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Njombe inayashikilia Magari makubwa 8 yaliyosheheni mizigo ya Mbao kwa makosa ya kukwepa kulipa Kodi.

Hayo yamesemwa na Meneja wa TRA mkoani Njombe, Mussa Shaaban ambapo amesema kuwa malori hayo yanashikiliwa kwa makosa ya kukwepa kodi na kutokuwa risiti za manunuzi.

Amesema kuwa wameyakamata malori kwasababu kuu mbili na sababu ya kwanza ni kutokuwa na risiti za manunuzi, huku kosa la pili akilitaja kuwa ni ukwepaji wa ulipaji kodi ambayo kimsingi inatakiwa kulipwa.

”Magari haya yote mnayoyaona ni magari mawili tu tumekuta yana risiti hizo za mashine na kwa mujibu wa sheria ukikamatwa kama tulivyowakamata hawa faini yake haipungui shilingi milioni tatu na isiyozidi milioni nne na nusu na hawa watatoa tu,”amesema Shaaban

Aidha, kwa upande wao baadhi ya wamiliki na madereva wa malori hayo akiwemo Godfrey Mhelela wamekiri kushikiliwa kwa makosa hayo hususani kutokuwa na uthibitisho wa mzigo unakotoka uliothibishwa na mtendaji husika.

Hata hivyo, vitendo vya ukwepaji kodi kwa wafanyabiashara na wasafirishaji wa mazao yanayotokana na misitu (mbao) wakishirikiana na watendaji wa kata na vijiji vimekuwa vikiendelea wilayani Njombe ambapo siku chache zilizopita katika kikao cha baraza la madiwani halmashauri ya wilaya ya Njombe, mwenyekiti wa halmashauri hiyo Valentino Hongoli alikemea vitendo hivyo na kuahidi kuchukuliwa hatua kali dhidi ya mtendaji yeyote atakayebainika kuhusika na utoroshwaji wa mapato.

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Februari 1, 2019
Mbowe, Matiko waendelea kusota rumande