Vikosi vya usalama vya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo vilirusha mabomu ya machozi na kupigana vita katika mitaa ya mji mkuu Kinshasa huku waandamanaji wanaoipinga serikali wakiandamana kwa madai ya ukiukwaji wa uandikishaji wapiga kura.

Waandamanaji hao pia wamekasirishwa na kupanda kwa gharama ya maisha na ukosefu wa usalama wa muda mrefu mashariki mwa nchi hiyo, ambapo wanamgambo wenye silaha na makundi ya waasi wameua mamia na wengine zaidi ya milioni moja kuyakimbia makazi yao.

Takriban waandamanaji dazeni walizuiliwa na vikosi vya usalama mara tu baada ya kuanza kwa maandamano hayo, ambayo yaliitishwa na viongozi wa upinzani.

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Kinshasa, Picha na REUTERS/ Thomas Mukoya

Msemaji wa polisi Sylvano Kasongo ameliambia shirika la habari la Reuters kuwa polisi watatu wamezuiliwa kwa vurugu dhidi ya mtoto mdogo wakati wa maandamano na kuongeza kuwa maafisa 27 wa polisi walijeruhiwa wakati wa mapigano hayo.

Waziri wa haki za binadamu wa Kongo Albert-Fabrice Puela, katika taarifa yake Jumamosi, alilaani ghasia za vikosi vya usalama dhidi ya waandamanaji na watoto wadogo, na kutaka uchunguzi ufanyike.

Kongo inatazamiwa kufanya uchaguzi mkuu Desemba 20 wakati Rais Felix Tshisekedi anatarajiwa kuwania muhula wa pili.

Lakini mvutano wa kisiasa unazidi kuongezeka katika mzalishaji mkuu wa cobalt duniani, huku baadhi ya wagombea wa upinzani wakilalamikia ucheleweshaji na madai ya ukiukwaji wa taratibu katika harakati za kusajili wapiga kura.

Viongozi wanne wa upinzani akiwemo Martin Fayulu, aliyeshika nafasi ya pili katika uchaguzi wa urais wa 2018, na Moise Katumbi, mfanyabiashara milionea na gavana wa zamani wa eneo anayetarajiwa kugombea 2023, waliitisha maandamano siku ya Jumamosi.

“Inasikitisha, unaona, wanarusha mabomu ya machozi. Hapo awali, ilikuwa risasi halisi,” Katumbi aliwaambia waandishi wa habari karibu na eneo la maandamano.

Fayulu alisema kwa njia ya simu kuwa gari lake lilikuwa limezingirwa na vikosi vya usalama vilivyoendelea kurusha mabomu ya machozi kuwatawanya waandamanaji.

“Daftari la uchaguzi si la kutegemewa na hatutaafikiana kuhusu suala hili,” Fayulu aliongeza.

Tume ya uchaguzi nchini Kongo inatarajiwa kuchapisha data ya usajili wa wapiga kura leo Jumapili.

Jeshi la Sudan, RSF kusitisha mapigano kwa siku saba
TAKUKURU yanusa rushwa fedha za Halmashauri