Manaibu Mawaziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano wamefanya ziara ya kutembelea na kukagua kiwanja kilichotolewa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya Wizara hiyo ambapo Serikali imetoa shilingi bilioni moja kwa kila Wizara na kuelekeza kuwa ifikapo mwishoni mwa mwezi Desemba mwaka huu Wizara zote ziwe zina majengo yake ya ofisi kwenye mji wa Serikali uliopo Ihumwa mkoani Dodoma

Naibu Waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa akiambatana na Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akiwa na Katibu Mkuu wa Mawasiliano Mhandisi Dkt. Maria Sasabo na wataalamu wa Wizara hiyo wametembelea na kukagua eneo lenye ukubwa wa ekari 6.3 ambalo limetengwa na Serikali kwa ajili ya ujenzi.

Aidha, Kwandikwa amesema kuwa Serikali imewapa dhamana kubwa ya kuwa wakandarasi na kusimamia majengo ya Wizara zote.

“Sisi kama Wizara tujenge vizuri kweli kweli ili tuwe mfano wa kuigwa na Wizara nyingine na tusimamie wakandarasi wengine wa JKT, NHC ambao wamepewa jukumu la kujenga ofisi za Wizara nyingine kwa kuwa sisi ndio wenye dhamana ya kusimamia wakandarasi wote nchini,”amesema Kwandikwa

Naye Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiiano Mhandisi Atashasta Nditiye ameiomba Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dodoma iweze kufikisha maji ya kutosha kwenye eneo hilo kwa ajili ya kufanikisha shughuli za ujenzi ii ziweze kukamilika kwa wakati uliopangwa na Serikali.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Mawasiliano Mhandisi Dkt. Maria Sasabo wakati akiwaonyesha Nditiye na Kwandikwa eneo hilo la ujenzi amesema kuwa ofisi hizo zitatumika kwa ajili ya Waziri, Manaibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, Naibu Katibu Mkuu na baadhi ya Wakurugenzi wa Wizara hiyo.

 

 

Serikali yafuta mitihani ya kidato cha pili
Morali ya kufanya kazi ya Kibunge imepungua- Godbless Lema