Mwanasiasa na tajiri mkubwa jijini Dar es Salaam, Yusuf Manji amekutana na pingamizi lingine kuhusu umiliki wa Ufukwe wa Coco (Coco Beach) baada ya Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kukata rufaa jana kwenye Mahakama ya Rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu uliomkabidhi mfanyabiashara huyo haki ya kuendeleza ufukwe huo kupitia kampuni yake ya Q Consult Ltd.

Maombi ya rufaa yaliwasilishwa kwa Msajili wa Mahakama ya Rufaa na timu ya viongozi wa Manispaa ya Kinondoni ambao ni Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Hapi, Meya wa Manispaa hiyo, Boniface Jacob, Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea na mshauri wa masuala ya sheria wa Manispaa hiyo.

Katika maombi yao ya rufaa, Manispaa hiyo inaiomba Mahakama ya Rufaa kubatilisha uamuzi wa Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi uliotoa haki ya umiliki kwa Manji pamoja na kutaka Manispaa imlipe shilingi milioni 500 kama fidia ya gharama za uendeshaji kesi.

Manispaa ya Kinondoni inapinga uamuzi wa Mahakama Kuu kwa madai kuwa ilitoa uamuzi huo ili hali ikijua dhahiri kuwa Manji alikuwa amevunja mkataba aliopewa.

“Jaji wa Mahakama Kuu kitengo cha Ardhi alitoa uamuzi huo wakati akijua [Yusuf Manji] alikuwa amevunja mkataba uliokuwepo. Ni muhimu kwa Mahakama ya Rufaa kubadilisha uamuzi huo,” Mshauri wa Sheria wa Manispaa hiyo aliwaambia waandishi wa habari.

Manispaa hiyo iliwasilisha maombi ya rufaa ikiwa ni saa chache kabla ya kufikia ukomo wa muda wa siku 90 waliopewa na mahakama Kuu kukata rufaa tangu uamuzi wa awali ulipotolewa.

 

Picha za kwanza za Mabaki ya Ndege ya EgyptAir iliyopotea zawekwa wazi
Video: Manny Pacquiao ashinda Useneta, Atajwa kuwa Rais wa Ufilipino ajaye