Msemaji  na Mkuu wa Habari klabu ya Simba, Haji Manara amesema golikipa bora zaidi nchini kwa sasa Aishi Salum Manula kesho, 1 agosti, 2017 anatarajiwa kujiunga rasmi na kambi ya klabu ya Simba iliopo Johannesburg, nchini Afrika Kusini.

Manula, amesaini mkataba wa miaka miwili kuitumikia klabu hiyo akimfuata straika, John Bocco ambaye kitambo kamwaga wino.

Manara amesema Manula amekamilisha taratibu zote za kujiunga na klabu ya simba na ameahidi kuwapa furaha wanachama na mashabiki wa timu hiyo ya Simba, ikiwemo kuisaidia klabu kushinda mataji yatakayowaniwa msimu huu.

Kipa huyo anakuwa mchezaji wa pili kuondoka Azam FC katika muda wa wiki moja na nusu baada ya aliyekuwa nahodha wake, Bocco, naye kusaini miaka miwili Simba wiki iliyopita.

Manula amekuwa katika kiwango cha juu katika kipindi cha miaka minne sasa ambapo mbali na kushinda tuzo ya Kipa Bora wa Ligi Kuu mara mbili (2016 na 2017), alikuwa kipa namba mbili Kombe la Kagame mwaka 2015.

Aidha Manara ametoa ratiba ya mechi zitakazochezwa na timu ya Simba nchini humo, ambapo Simba kesho inatarajiwa kucheza mechi ya kwanza ya maandalizi ya msimu dhidi ya mabinga wa zamani wa Afrika Orlando Pirates ya nchini Afrika Kusini.

Orlando ni klabu maarufu nchini Afrika Kusini imeahidi kushusha silaha zake muhimu ili kuwapa Simba maandalizi ya kutosha katika mchezo huo unaotarajiwa kuchezwa nchini kwao, Afrika kusini.

Mechi nyingine ya mwisho itachezwa na Simba nchini huko dhidi ya mabingwa wa soka nchini kwa sasa Bidvest.

NEC yaitahadharisha CUF, yajibu mapigo kuhusu tuhuma
Video: Barrick watua Ikulu, mjadala wa makinikia waanza rasmi Dar