Marekani imesema kuwa inawatuma wanajeshi 5,200 kusaidia kulinda mipaka kati ya nchi hiyo na Mexico, baada ya maelfu ya wahamiaji kutoka mataifa ya Amerika ya Kati kujiunga na msafara wa wahamiaji unaoelekea Marekani.

Idadi hiyo ya wanajeshi wanaotumwa kuulinda mpaka ni kubwa kuliko ilivyotarajiwa huku Rais Donald Trump akizidi kuwa na misimamo mikali kuhusu uhamiaji kuelekea chaguzi za katikati ya muhula zinazotarajiwa kuanza tarehe 6 mwezi Novemba.

Jenerali Terrrence O’ Shaughnessy, anayesimamia kambi ya wanajeshi walioko Kaskazini mwa Marekani amesema kuwa wanajeshi 800 tayari wako njiani kueleka katika mpaka wa Texas na wengine wanaelekea katika mipaka ya California na Arizona, ambapo ameongeza kuwa Rais Trump ameweka wazi kuwa ulinzi wa mipaka ni jambo la usalama wa kitaifa.

Aidha, wakati hayo yakijiri, mamia ya wahamiaji kutoka Honduras wamevuka mto kuingia Mexico, hilo likiwa kundi jipya la wahamiaji wanaoelekea Marekani ambapo kulingana na taarifa kutoka Umoja wa Mataifa imesema kuwa zaidi ya wahamiaji 7,000 wako njiani kuelekea Marekani.

Hata hivyo, katika kampeni za uchaguzi wa rais mwaka 2016, Trump alitumia suala la uhamiaji haramu kama mojawapo ya ahadi atakazozipa kipaumbele akiingia madarakani, na sasa anatumia suala la msafara wa wahamiaji kutoka mataifa ya Amerika ya Kati kukipigia debe chama chake cha Republican katika uchaguzi wa katikati ya muhula.

 

Moto wa ajabu wateketeza kanisa, picha ya Yesu yasalia
Ray C amshika mkono Wema, "Bado nina imani na wewe"