Marekani imetaka kusitishwa kwa mapigano nchini Yemen na kufanyika mazungumzo ya amani huku muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia ukituma majeshi 10,000 zaidi kuelekea mji wa Hodeida unaodhibitiwa na waasi.

Waziri wa ulinzi wa Marekani, Jim Mattis ametaka kuwepo makubaliano ya kusitisha mapigano nchini Yemen na pande zinazo zozana kufanya mazungumzo katika kipindi cha siku thelathini zijazo.

Amesema kuwa Marekani imekuwa ikiutizama mzozo wa Yemen kwa muda wa kutosha na anaamini kuwa Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu ambao ni washirika muhimu wa muungano wa kijeshi unaoungwa mkono na Marekani dhidi ya waasi wa Houthi wako tayari kwa mazungumzo.

Aidha, waziri huyo amesema kwamba muda umewadia wa kufanya mazungumzo ya kutafuta amani na kuzitaka pande zinazo zozana kukutana na mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Yemen, Martin Griffiths nchini Sweden mwezi ujao ili kufikia suluhisho.

Hata hivyo, Marekani imekuwa ikishutumiwa vikali kwa kuunga mkono muungano huo wa kijeshi unaoongozwa na Saudia hasa baada ya mashambulizi kadhaa ya angani kuwalenga raia.

 

Watakaoivaa Bafana Bafana, Uganda watajwa
Tajiri wa PSG kushughulikia usajili wa Paul Pogba