Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni amemtaja Katibu wa Tume ya Dawa za Kulevya Zanzibar, Heriyangu Mgeni kuwa ni mmoja wa wanaokwamisha juhudi za serikali katika kupambana na dawa hizo nchini.

Ameyasema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari Visiwani Zanzibar, ambapo amesema kuwa atatoa mapendekezo kwa mamlaka inayohusika na mapambano ya dawa hizo kumuondoa katika nafasi yake kutokana na uzembe anaoufanya.

“Mimi nikiwa na dhamana, mara kadhaa nimekuwa nikimuita Katibu nikishauriana naye kwa kuwa suala la dawa za kulevya linaniumiza roho, ni mpaka leo Kisiwa cha Zanzibar chenye watu milioni 1.3 kinashindwa kupambana matatizo ya dawa za kulevya kwa kiwango kinachostahili,” amesema Masauni.

Aidha Naibu Waziri huyo amesema kuwa haoni kama Zanzibar ina nia ya dhati ya kupambana na dawa za kulevya kwa aina ya Katibu huyo aliyedai anakwamisha juhudi za serikali.

Hata hivyo, ameongeza kuwa amegundua kuna mapungufu ya baadhi ya askari kwa kuwa wapo wanaoharibu kesi za dawa za kulevya makusudi kwa kuchukua rushwa kutoka kwa wauzaji wa dawa hizo wanaojulikana na kuwaachia mitaani na amemwelekeza Katibu wa Wizara hiyo kuunda tume maalumu itakayokuja kufanya kazi Zanzibar kuwabaini askari wanaozorotosha jambo hilo na hatua za haraka zichukuliwe.

Video: Maaskofu watoa maneno mazito, Agizo la JPM ujenzi wa stendi kaa la moto Njombe
Muro atoa onyo kali, 'Hatutakupa dhamana'