Serikali imezitahadharisha Kampuni Binafsi za Ulinzi kutoshiriki katika matukio ya uhalifu baada ya kuripotiwa mara kwa mara kwa walinzi wa kampuni hizo kupatikana na hatia ya uhalifu mahala pa kazi ikiwemo kuwaazima silaha wahalifu kwenda kufanya matukio ya uhalifu.

Hayo yamesemwa jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Chama cha Sekta ya Ulinzi Tanzania (TSIA).

Amesema kuwa kampuni zinatakiwa kuongea na walinzi wao sambamba na kuongeza maslahi kwa walinzi hao ili wasiingie katika vishawishi hali itakayopelekea kutoshiriki katika matukio ya uhalifu sehemu zao za kazi.

“Baadhi ya walinzi wa kampuni mnazozisimamia wamekua wakishiriki katika uhalifu, wengine wameenda mbali zaidi kwa kuwaazima silaha wahalifu kwenda kufanyia uhalifu, jambo hili halikubaliki, sasa naziagiza kampuni zenye walinzi wa namna hii kuhakikisha vitendo hivi vinakoma mara moja,” amesema Masauni

Akizungumza kwa niaba ya Jeshi la Polisi, Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Narcis Misama amesema kuwa wao kama jeshi wanawahakikishia wanachama hao wa sekta ya ulinzi ushirikiano utakaowasaidia kutimiza majukumu yao huku akiweka wazi jeshi kama jeshi haliwezi kuyafikia maeneo yote kwa wakati.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Sekta ya Ulinzi Tanzania, Felix Kagisa aliiomba serikali ipitishe sheria zinazoongoza sekta ya ulinzi binafsi ili waweze kufanya kazi zao kwa mujibu wa sheria na taratibu  za nchi.

BOT yafunga benki nyingine
HESLB yaja kivingine, yawaweka mtegoni wanufaika wa mikopo