Mashabiki na wanachama wa klabu ya Simba wameombwa kujitokeza kwa wingi katika mchezo wa ligi dhidi ya watani wao wa jadi Young Africans siku ya Jumapili ili kuwapa sapoti wachezaji wao.

Mchezo huo wa mzunguko wa pili wa ligi utafanyika katika uwanja wa Taifa huku Wekundu hao wakiendelea kuongoza msimamo wa ligi hiyo kwa tofauti ya pointi 11, dhidi ya Young Africans wanaoshika nafasi ya pili.

mkuu wa idara ya habari na mawasilino wa klabu ya Simba, Hajji Sunday Manara ametoa wito huo kwa mashabiki na wanachama, alipozungumza na waandishi wa habari leo mchana makao makuu, mtaa wa Msimbazi.

Manara amewataka mashabiki na wanachama kununua tiketi kwa mawakala wa Selcom ili kuhakikisha wanahudhuria kwa wingi mchezo huo, ambao unatazamwa kama hakimu wa kuamua Simba kutwaa ubingwa, ama kusubirishwa na Young Africans wanaotaka kutetea kwa mara ya nne mfululizo.

Manara amewaasa mashabiki na wanachama kuacha kununua tiketi kwa watu binafsi kwakua wanaweza kuuziwa tiketi feki na wakashindwa kuingia uwanjani hali ambayo itasababisha vurugu.

“Niwaombe mashabiki wetu kuja kwa wingi uwanjani Jumapili kutoa sapoti kwa wachezaji ili tupate ushindi, tena wahahakishe wananua tiketi kwa mawakala wa Selcom kwa ajili ya kuondoa usumbufu,” alisema Manara.

katika hatua nyingine Manara amewaasa mashabiki watakaojitokeza uwanjani kujizuia na jazba hata kama watakuwa hawajatendewa haki na mwamuzi ili kudumisha amani.

Wakati huo huo Mkuu huyo wa kitengo cha habari na mawasiliano cha klabu ya Simba, amewaasa Watanzania hasa Waandishi wa habari kutotumia neno MAHASIMU kwa kulihusiha na klabu kongwe hapa nchini (Simba na Young Africans).

Manara amesema neno mahasimu lina maanisha VITA au UADUI kitu ambacho sio kweli na kinapaswa kupingwa kwa nguvu zote.

Manara ameongeza kuwa “Simba na Young Africans sio mahasimu ni watani wa jadi, na ndio maana tuna taniana, tunasaidiana masuala mbalimbali tungekuwa mahasimu jambo hili lisingetokea.

“Nawaomba waandishi wa habari kuacha kutumia neno hilo kwakua linatugombanisha na wadau wetu. Ugomvi wa Simba na Yanga ni ndani ya dakika 90 tu zikiisha tunarudi kwenye utani wetu,” alisema Manara.

Simba waatakuwa mwenyeji wa Young Africans katika uwanja wa Taifa siku ya Jumapili kwenye mchezo wa mzunguko wa pili wa ligi kuu.

Paul Makonda mgeni rasmi Simba SC Vs Young Africans
Bodi ya Filamu nchini Kenya yapiga marufuku filamu inayohusu ushoga