Kaimu kocha mkuu wa Simba Sc Seleman Matola amesema hafahamu lolote kuhusu maradhi ya ‘MSHIPA WA NGIRI’ yanayotajwa kumsumbua kiungo mshambuliaji kutoka nchini Ghana Bernard Morrison.

Kiungo huyo anatajwa kusumbuliwa na maradhi hayo, na huenda ikamchukua muda wa miezi sita kupona, na kisha kurejea tena dimbani kujiunga na wachezaji wenzake wa Simba SC.

Matola amesema taarifa za kiungo huyo ambaye aliongozana na kikosi cha Simba SC kuelekea visiwani Zanzibar kwa ajili ya ushiriki wa michuano ya Kombe la Mapinduzi, kusumbuliwa na maradhi ya ‘MSHIPA WA NGIRI’ amekua akizisika kama ilivyo kwa wadau wengine wa michezo nchini.

Amesema anachokifahamu ni kwamba Morrison alikua anasumbuliwa na Malaria, lakini wakati anakwenda Zanzibar alikua ameshapona na ndio maana aliamua kumjumuisha kwenye kikosi chake.

“Sifahamu lolote kuhusu maradhi ya ‘’MSHIPA WA NGIRI’ yanayotajwa kumsumbua Morrison, mimi ninafahamu alikua anaumwa na Malaria na alikua ameshapona, ndio maana niliamua kumjumuisha kwenye kikosi kilichokwenda Zanzibar.”

“Suala la kusumbuliwa na ‘MSHIPA WA NGIRI’ linaweza kuthibitishwa na madaktari, lakini mimi kama kocha, siwezi kusema lolote juu ya hilo ambalo kwa sasa kila mtu analizungumza.”

Katika hatua nyingine Matola ametoa sababu za kushindwa kumtumia Morrison kwenye michuano ya Kombe la Mapinduzi, kwa kusema mchezaji huyo hakuwa timamu kimwili ‘FIT’ kwa kucheza kwa dakika 90.

“Morrison hakuwa timamu kimwili kutokana na maradhi yaliyokua yakimsumbia (Malaria), lakini nilimchukua ili aweze kurejesha utimamu wa kimwili kwa kufanya mazoezi ya wachezaji wenzake, ninashukuru aliweza kufanya hivyo na aliniomba kucheza kwa dakika 10 katika mchezo wa fainali lakini sikumpa nafasi hiyo, kutokana na sababu za kiufundi.”

Matola anaendelea kukaimu nafasi ya kocha mkuu Simba SC, hadi Uongozi utakapokamilisha mchakato wa kumpata na kusaini mkataba na kocha mpya, atakaerithi mikoba ya Sven Vanderbroek.

Daktari: Carlinhos 'SAFI', Yacouba 'BADO'
Azam FC kumaliza na Kombaini ya Zanzibar