Mawaziri sita wawekwa kikaangoni kutokana na kile kilichonukuliwa kuwa ni utendaji mbovu unaoleta matokeo mabovu katika wizara  zao, mawaziri hao ni Joyce Ndalichako, Hamisi Kingwangalla, Mwigulu Nchemba, Luaga Mpina, Isaack Kamwelwe na Philip Mpango.

Ambapo wabunge wamelalamikia sekta zinazoendeshwa na mawaziri waliotajwa hapo juu na kusema kwamba hawafanyi vizuri katika sekta zao.

Hamisi Kingwangalla, Waziri wa Maliasili na Utalii amelaumiwa na kamati ya Bunge ya Ardhi kwa kufuta leseni zote za umiliki wa vitalu kwa mwaka 2018-2022 zilizotolewa kihalali na Wizara, Kutokana na uamuzi huo kamati imeliomba Bunge kuunda kamati ndogo ya uchunguzi ili ijiridhishe mikakati iliyochukuliwa na Serikali ya kugawa Vitalu vya uwindaji kwa njia ya mnada imesaidia kuongeza pato la taifa.

Mwigulu Nchemba, Waziri wa Mambo ya Ndani, wizara yake imelaumiwa juu ya mradi wa pasi mpya za kusafiria, ambapo imesemekana kuwa Serikali imedanganya Umma kupitia mradi wake mpya wa Pasi za kielektroniki na kupanda kwa gharama za vitambulisho vya taifa, maelezo ambayo amedai yametokana na taarifa ya Kamati ya Hesabu za serikali PAC, hoja hii iliibuliwa na Mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche.

Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia analaumiwa kwa matokeo mabaya katika shule za Serikali kulinganisha na shule binafsi zinazofanya vizuri katika mitihani Kitaifa na kushika nafasi nzuri ya kuingia kumi bora hali ambayo ni tofauti kwa shule za serikali ambazo zimekuwa zikishia mkia na kutokufanya vizuri katika mfululizo wa miaka kadhaa sasa kutokuingia katika shule kumi bora zinazofanya vizuri, hoja hii imeibuliwa na  Mlinga na kumtaka Rais Magufuli kumtengua katika kiti hiko.

Luaga Mpina, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, analaumiwa kwa kutoa majibu mepesi kuhusu hoja ya kukamatwa kwa samaki wanaodaiwa kuvuliwa kwa njia haramu.

Hayo yaliibuliwa katika Bunge la 11 kikao cha 10 kilichofanyika jana Jijini Dodoma, ambapo Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, alipata nafasi kujibu maswali mbalimbali yaliyokuwa yakiulizwa na wabunge bungeni hapo.

Video: Mwalimu amtakia Mtulia ‘kila la kheri’
Jaji atakiwa kuondolewa kwa kutomfunga jela mbakaji wa mtoto asiyeona