Mshambuliaji tegemeo wa Kikosi cha Mabingwa wa Soka Tanzania Bara Young Africans Fiston Kalala Mayele amesema, bado ana kiu ya kufunga mabao katika Mshike Mshike wa Ligi Kuu msimu huu 2022/23.

Mayele alifunga mabao mawili wakati wa mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Mbeya City FC Jumamosi (Novemba 26), na kumfanya kufikisha idadi ya mabao saba katika michezo mitatu mfululizo aliyocheza mwezi huu.

Mshambuliaji huyo kutoka DR Congo amesema licha ya kufungwa idadi hiyo ya mabao, lakini kwake bado ataendelea kupambana ili kuhakikisha anafunga zaidi na kuisaidia timu yake kufikia malengo ya kupata alama tatu za kila mchezo.

“Nafahamu kuwa ni idadi kubwa ya mabao, mabao saba katika michezo mitatu ni namba nzuri ukiwa kama Mshambuliaji, kwa upande wangu namshukuru Mungu kuona ninazidi kuifungiaYoung Africans mabao mengi.”

“Kikubwa ni mimi kuona naendelea kuzitumia nafasi za mabao ambazo ninazipata, naamini kila kitu kitakuwa sawa, Mashabiki, Viongozi, Benchi la Ufundi na hata sisi wachezaji tunatamani kuona kila mara tunapata matokeo mazuri, na mwisho wa msimu tuweze kuwa mabingwa.” amesema Mayele

Mayele alifunga mabao matatu dhidi ya Singida Big Stars Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam, kisha akaifunga Dodoma jiji FC katika Uwanja wa Liti mkoani Singida na juzi Jumamosi (Novemba 26) alifunga mawili dhidi ya Mbeya City.

Azam Complex kufanyiwa maboresho
QATAR wamtumia Mesut Ozil kulipa kisasi