Mwenyekiti wa chama cha NCCR -Mageuzi James Mbatia na makamu Mwenyekiti (Bara), Angelina Mtahiwa wamesimamishwa kutojihusisha na shughuli zozote za chama kutokana na tuhuma mbalimbali zinazowakabili.

Uamuzi huo umefikiwa leo Mei 21, 2022 na Halmashauri Kuu ya chama hicho kutokana na viongozi hao kukabiliwa na tuhuma za kuwagombanisha viongozi kuwalazimisha kujiuzulu na tuhuma nyingine.

Mjumbe wa Halmashauri Kuu na Mwenyekiti wa azimio la kusimamishwa kwa viongozi hao Joseph Selasini amesema pamoja na hatua hiyo pia wamelivunja Baraza la Wadhamini la NCCR na kuteua wajumbe wapya ambao watasajiliwa kwa mujibu wa taratibu zitakazowekwa.

“Viongozi hawa wamesimamishwa hadi mkutano Mkuu utakapoitishwa ili wajieleze kuhusiana na tuhuma zinazowakabili na hii ni kutokana na tabia ya kukosa uaminifu,” amesema Joseph Selasini.

Naye Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini Sisty Nyahoza amesema tayari amepokea barua kutoka NCCR-Mageuzi ikijulisha mabadiliko ya wajumbe wa bodi ya wadhamini.

“Pamoja na mabadiliko hayo kulikuwa na ajenda nyingine ambayo ni kusimamishwa kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti Bara kutokana na maazimio hayo hivyo tunasubiri barua rasmi ili kutoa taarifa,” amefafanua Nyahoza.

Mbatia ni miongoni mwa wanasiasa wachache waliodumu kwenye siasa za Upinzani Tanzania akiwa miongoni mwa wenye viti wenza wa umoja ulioitwa UKAWA uliondwa kwa pamoja na vyama vingine vya upinzani kama CUF na CHADEMA.

Wahariri chanzo ukuaji wa biashara
Rais Samia amuapisha Mwalimu wake