Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amezungumza kwa mara ya kwanza baada ya kuachiwa huru pamoja na viongozi wengine sita wa Chadema na kusema kuwa walipokuwa magerezani wameshuhudia mengi na watayaweka wazi karibuni waliyoyashuhudia ndani ya siku saba walizokuwa Segerea.

Mbowe amesema hayo alipokuwa nje ya Mahakama ya Hakimu mkazi Kisutu baada ya kukamilisha masharti ya dhamana ambapo kila mmoja alitakiwa kuwa na wadhamini wawili pamoja na kusaini bondi ya shilling Million 20.

“Leo mahakama imetupa ruksa ya dhamana na tunaanza dhamana yetu siku ya leo kwa mashtaka ambayo yananikabili mimi na wenzangu, tumekuwa gerezani Segerea kwa siku saba mimi na wenzangu na tunamshukuru Mungu tuko salama mimi na wenzangu na tumewaona Watanzania wengi zaidi ya elfu mbili ndani ya gereza la Segerea ambao wengi wao haki yao imecheleweshwa kwa hiyo tunasema ni haki iliyominywa, tutazungumza mengi tuliyoyaona Segerea na baadaye tutatoa taarifa rasmi ya chama kuhusiana na kesi hii” amesema Mbowe

Aidha Mbowe aliendelea kusema kuwa

“Zamani tuliona nchi hii ina udikteta uchwara ila sasa ina udikteta kamili, tutayazungumza na kutolea ufafanuzi kamili katika muda muafaka” amesema Mbowe.

Aidha Mbowe na viongozi wenzake sita walishikiliwa na polisi kufuatia kesi inayowakabili ya kuhamasisha maandamano yaliyosababisha kifo cha mwanafunzi wa chuo cha usafirishaji cha NIT, Akwilimna Akwiline.

Viongozi hao walitiwa mbaroni tangu walipopandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka Machi 27, 2018.

Afrika kusini yaomboleza kifo cha Winnie Mandela.
Video: Askofu anusurika kuuawa kwa panga madhabauni